CUF yasikitishwa na matukio ya mabomu



 Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar Mhe. Nassor Ahmed Mazrui akizungumza na vyombo vya habari kuhusiana na matukio ya miripuko ya mabomu.
Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Timu ya Ushindi CUF Mhe. Ismail Jussa Ladhu, akimkaribisha Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho Mhe. Nassor Ahmed Mazrui (kulia), kuzingumza na waandishi wa habari katika ofisi za Chama hicho Mtendeni Zanzibar. (Picha na OMKR)

Na: Hassan Hamad, OMKR

Chama Cha Wananchi CUF, kimeelezea kusikitishwa na matukio ya kuwatia hofu wananchi na kuhatarisha amani ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za Chama hicho Mtendeni Zanzibar, Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar Nassor Ahmed Mazrui, ameyataja matukio hayo kuwa ni pamoja na miripuko inayoelezwa kuwa ni mabomu katika maeneo ya Mkunazini na Michenzani.

Ameyataja matukio mengine kuwa ni uvamizi uliofanywa katika kisiwa cha Tumbatu ambao ulipelekea nyumba nne kutiwa moto na nyengine kadhaa kuvunjwa, sambamba na kupigwa na kujeruhiwa kwa wananchi 16 wa kisiwa hicho.

Akifafanua kuhusu matukio ya miripuko, Mhe. Mazrui ameishauri Serikali kuwatafuta waliotega mabomu hayo kwa kutumia picha za kamera za ulinzi za CCTV ambazo zimesambazwa katika eneo lote la Mji Mkongwe.

Amesema bila ya kuchukuliwa kwa hatua wananchi wataendelea kuamini kuwa matukio hayo yamepangwa makusudi kwa lengo la kuwatia hofu wananchi washindwe kuendelea na shughuli zao za kimaisha.

Wakati hayo yakiendelea, Mhe. Mazrui amesema juhudi kubwa zimeanza na zinaendelea vyema kwa kuzishirikisha jumuiya na taasisi za ndani na nje ya nchi, zikiwa na lengo la kukwamua mkwamo wa kisiasa unaoikumba Zanzibar hivi sasa.

Nae Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Timu ya Ushindi CUF Mhe. Ismail Jussa Ladhu, amesema wanatiwa moyo na juhudi zinazoendelea, na kuwataka wananchi kuendelea kuwa wavumilivu na kudumisha amani.

Post a Comment

Previous Post Next Post