Daktari: Ray kupata magonjwa 10 hatari kama anatumia mkorogo

Na Mwandishi Wetu, AMANI
DAR ES SALAAM: Lile sakata la nyota wa sinema Bongo, Vincent Kigosi ‘Ray’ kudai kwamba, siku hizi amekuwa mweupe pee kwa sababu ya kunywa sana maji na kufanya mazoezi, limechukua sura mpya kufuatia daktari mmoja jijini Dar kusema mwongozo huo ni upotoshaji mkubwa, Amani linakupa zaidi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi juzi, daktari wa kituo cha kutoa huduma za afya kilichopo Kimara jijini Dar, Godfrey Chale alisema binadamu kunywa maji kwa wingi, hata kiasi cha pipa kwa siku moja, hakusababishi kuwa mweupe.
rayyyyyy.jpg“Mtu akinywa maji kwa wingi na kufanya mazoezi anapata faida ya kuifanya ngozi yake kuwa nyororo zaidi. Na wengi wanaofanya hivyo ni wale wanaopoteza hali ya kuzeeka. “Lakini weupe siku zote unatokana na kujichubua. Ila sasa, madhara ya kujichubua ni mengi. Wanaojichubua wanakuwa katika hatari ya kupata magonjwa kama kumi hivi.
“Kwanza wanaweza kupata kansa ya ngozi, chunusi kwa wingi, uvimbe kwenye ngozi, ngozi kuwa nyembamba, kuongezeka kwa hamu ya kula na uzito, kutokwa na mabakamabaka mwilini, kupata pumu na kuzaa watoto wenye kasoro.
“Lakini pia wanaweza kupata magonjwa ya akili, kuharibika kwa maini, kuharibika kwa mishipa ya fahamu na figo kwa sababu ya wingi wa mercury (zebaki) inayokuwa kwenye vipodozi. Pia wanaweza kupata tatizo la kupungua kwa uzito wa mifupa hivyo kuwa katika hatari ya mifupa hiyo kuvunjika. Madhara haya huonekana mara moja lakini pia yanaweza kujitokeza kadiri mtu anavyoendelea kujichubua.
Juzi Amani lilimsaka Ray kwa njia ya simu yake ya kiganjani na kumpa salamu hizo ambapo alisema: “Huyo dokta amesema tu, lakini sidhani kama anafahamu. Mimi weupe wangu unatokana na kunywa maji kwa wingi na mazoezi.

“Halafu pia isitoshe, katika ukoo wetu hakuna mtu mweusi. Kwa hiyo mimi kuwa mweupe ni jambo la lazima,” alisema Ray ambaye mpaka sasa hajawahi kubadili kauli yake ya kunywa maji ndiko kumemfanya awe mweupe sana.

Post a Comment

Previous Post Next Post