Na Mwandishi Wetu, AMANI
DAR ES SALAAM: Lile sakata la nyota
wa sinema Bongo, Vincent Kigosi ‘Ray’ kudai kwamba, siku hizi amekuwa
mweupe pee kwa sababu ya kunywa sana maji na kufanya mazoezi,
limechukua sura mpya kufuatia daktari mmoja jijini Dar kusema mwongozo
huo ni upotoshaji mkubwa, Amani linakupa zaidi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi
juzi, daktari wa kituo cha kutoa huduma za afya kilichopo Kimara jijini
Dar, Godfrey Chale alisema binadamu kunywa maji kwa wingi, hata kiasi
cha pipa kwa siku moja, hakusababishi kuwa mweupe.
“Mtu
akinywa maji kwa wingi na kufanya mazoezi anapata faida ya kuifanya
ngozi yake kuwa nyororo zaidi. Na wengi wanaofanya hivyo ni wale
wanaopoteza hali ya kuzeeka. “Lakini weupe siku zote unatokana na
kujichubua. Ila sasa, madhara ya kujichubua ni mengi.
Wanaojichubua wanakuwa katika hatari ya kupata magonjwa kama kumi hivi.
“Kwanza wanaweza kupata kansa ya ngozi,
chunusi kwa wingi, uvimbe kwenye ngozi, ngozi kuwa nyembamba, kuongezeka
kwa hamu ya kula na uzito, kutokwa na mabakamabaka mwilini, kupata
pumu na kuzaa watoto wenye kasoro.
“Lakini pia wanaweza kupata magonjwa ya
akili, kuharibika kwa maini, kuharibika kwa mishipa ya fahamu na figo
kwa sababu ya wingi wa mercury (zebaki) inayokuwa kwenye vipodozi. Pia
wanaweza kupata tatizo la kupungua kwa uzito wa mifupa hivyo kuwa katika
hatari ya mifupa hiyo kuvunjika. Madhara haya huonekana mara moja
lakini pia yanaweza kujitokeza kadiri mtu anavyoendelea kujichubua.
Juzi Amani lilimsaka Ray kwa njia ya
simu yake ya kiganjani na kumpa salamu hizo ambapo alisema: “Huyo dokta
amesema tu, lakini sidhani kama anafahamu. Mimi weupe wangu unatokana na
kunywa maji kwa wingi na mazoezi.
“Halafu pia isitoshe, katika ukoo wetu
hakuna mtu mweusi. Kwa hiyo mimi kuwa mweupe ni jambo la lazima,”
alisema Ray ambaye mpaka sasa hajawahi kubadili kauli yake ya kunywa
maji ndiko kumemfanya awe mweupe sana.
Post a Comment