Vigogo Jiji la Dar es Salaam Wakalia Kuti Kavu....Makonda Afichua Siri Mikataba Tata, Ataka Mamlaka za Uteuzi Ziwaondoe


Kamati maalumu ya uchunguzi iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda imefichua madudu na harufu ya ufisadi katika utekelezwaji wa mikataba mitatu, inayohusu maeneo ya ukusanyaji mapato ya Stendi Kuu ya Mabasi Yaendayo Mikoani ya Ubungo na kodi ya uegeshaji magari katikati ya mji.

Kutokana na madudu hayo, Mkuu huyo wa Mkoa amebainisha wazi kuwa hataki kufanya kazi tena na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Kabwe na Kaimu wake, Sarah Yohana na kuwasilisha majina yao kwa mamlaka husika ya nidhamu kwa hatua zaidi.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, alisema hivi karibuni aliunda kamati hiyo maalumu kufuatilia maeneo hayo muhimu kutokana na malalamiko ya muda mrefu, ambayo ofisi yake ilikuwa ikipokea kutoka kwa wananchi.

Alisema kwa mujibu wa uchunguzi, kamati hiyo ilibaini kuwa katika stendi ya mabasi ya Ubungo, kumekuwa na ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma, ikiwemo kutokuwasilishwa kwa mapato halisi yanayotokana na makusanyo ya kila siku serikalini.

“Kamati ile imebaini kuwa pale ubungo kunatumika sheria ndogo mbili za ukusanyaji mapato moja ya mwaka 2004 na nyingine mwaka 2009 kwa lengo la kunufaisha wachache,” alisema Makonda.

Alifafanua kuwa Sheria Ndogo ya Mwaka 2004 ya ukusanyaji mapato ndani ya kituo hicho, inaonesha kuwa kila basi linatakiwa kutozwa Sh 4,000, hivyo makusanyo halisi kwa mwezi ni Sh milioni 42 kutokana na mabasi 350 yanayoegeshwa kituoni hapo.

Hata hivyo, alisema kutokana na mabadiliko ya tozo, sheria hiyo ilibadilishwa mwaka 2009 na kila basi likawa linatozwa Sh 8,000 na hivyo makusanyo ya mwezi yakapanda na kufikia Sh milioni 82 kwa mwezi.

“Lakini cha kushangaza tumebaini kuwa bado kampuni inayokusanya mapato katika kituo cha Ubungo, inawasilisha mapato hayo kwa kutumia sheria ya mwaka 2004 yaani Sh milioni 42 badala ya Sh milioni 82 kwa mwezi…” 
“…Mbaya zaidi kamati ile katika ukaguzi wake, ilikuta kampuni ya ukusanyaji mapato hayo stendi ya Ubungo inayo Sheria ya Mwaka 2009 lakini katika nyaraka za Halmashauri ya Jiji zinaonesha sheria inayotumika ni ya mwaka 2004,” alisisitiza Makonda.

Alisema katika uchunguzi ilibainika kuwa kampuni iliyo chini ya Halmashauri ya Jiji inayokusanya mapato hayo stendi ya Ubungo, ilisaini mkataba wa ukusanyaji mapato hayo kwa mara ya kwanza Januari 31, 2004 na baadaye ikasaini tena mkataba Januari 30, mwaka jana.

Kwa mujibu wa Makonda, kwa hali ilivyo tangu Sheria Ndogo ya Mwaka 2009 ipitishwe, haijawahi kutumika na hivyo kulisababishia hasara jiji hilo ya Sh bilioni tatu kutokana na mapato katika stendi hiyo kuendelea kuwasilishwa kwa kutumia sheria ya mwaka 2004.

“Ukipiga hesabu za harakaharaka utagundua kuwa kila mwezi Sh milioni 42 zimekuwa zikipotelea kwenye mikono ya wachache, kwa maana hiyo kuanzia mwaka 2009 Sh bilioni tatu zimepotea na kila mwaka tumekuwa tukipoteza Sh milioni 500, huu ni ufisadi wa aina yake kwa kweli,” alisema.

Alisema wakati fedha hizo zikipotea kwenye mikono ya wachache, kamati hiyo pia ilibaini kuwa hali ni mbaya katika kituo hicho cha Ubungo kwani pamoja na ukosefu wa vyoo na maegesho bora kwa mabasi, lakini pia vibanda vya biashara vilivyomo ndani ya stendi hiyo, vimekuwa vikitumika kukandamiza maskini na kunufaisha wachache.

“Kwa mujibu wa taratibu, kila kibanda mle ndani ya stendi kinatakiwa kukodishwa kwa Sh 200,000 kwa mwezi, lakini tumebaini kuwa wapo watu wachache wamevihodhi na kuvikodisha kwa zaidi ya Sh milioni 1.5,” alisema.

Kuhusu mkataba wa maegesho katikati ya jiji kupitia Kampuni ya National Parking System (NPS), alisema kamati hiyo pia imebaini kuwa Halmashauri ya Jiji imeiongezea mkataba wa miezi 10 kampuni hiyo kinyume cha taratibu wakati mkataba wake ulikuwa umeshamalizika.

Alisema mara baada ya mkataba huo kumalizika Agosti mwaka jana Mkurugenzi wa Jiji, Kabwe aliiandikia barua kampuni hiyo na kuiongezea muda wa miezi sita kwa madai kuwa mchakato wa kutafuta mzabuni mpya pamoja na kwamba umeanza, haujakamilika.

Aidha, Kaimu Mkurugenzi Yohana naye aliandika miezi kadhaa baadaye barua na kuiongezea tena kampuni hiyo muda wa miezi minne iendelee kukusanya kodi ya maegesho kwa kuwa bado mchakato wa kutafuta mzabuni mpya haujakamilika.

“Barua zote mbili zina saini ya viongozi hawa wawili, hatua hizi ni kinyume kabisa na maadili ya viongozi pamoja na Katiba ya nchi. Haiwezekani mchakato wa kumtafuta zabuni uchukue zaidi ya miezi sita,” alieleza Makonda.

Pamoja na hayo, Makonda pia alisema kamati hiyo katika uchunguzi wake dhidi ya Kampuni ya Tambaza inayosimamia makosa ya pikipiki na maegesho ya magari katika sehemu zisizotakiwa, imekuwa ikitoza fedha nyingi za faini kinyume cha mkataba.

“Mkataba wao unaonesha wazi kuwa wanatakiwa wakikamata pikipiki yenye makosa watoze faini ya Sh 20,000 lakini imebainika wao wanatoza zaidi ya Sh 80,000. Licha hivyo pia mkataba unawataka wazingatie dharura na kutotumia lugha chafu lakini yote haya hawayazingatii,” alisema.

Alisema tangu Rais John Magufuli aingie madarakani amekuwa mstari wa mbele kupiga vita ubadhirifu wa fedha za umma, rushwa na ufisadi hivyo akiwa kama Msaidizi wa Rais anaunga mkono juhudi hizo ndio maana hawezi kunyamazia madudu yeoyote yanayohusu ufisadi.

“Nimewasiliana na mamlaka husika ya nidhamu ili ichukue hatua stahiki dhidi ya viongozi hawa wawili Kabwe na Yohana na nimeiambia mamlaka hii kwa uwazi kabisa siwahitaji kuendelea nao hapa Dar es Salaam,” alisisitiza.

Aidha, alisema tayari amewasiliana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuhusu mikataba hiyo yote mitatu ambayo imeahidi kuanza kuifanyia kazi leo.

Alisema ameamua kuchukua hatua hiyo ya kuwashughulikia wakurugenzi hao kwa kuwa wao ndio tatizo kwani mikataba hiyo hata ikivunjwa kwa sasa itakuwa ni kazi bure kama viongozi hao wataendelea kuwepo.

Hii ni mara ya pili kwa Stendi ya Ubungo kuingia katika kashfa ya ubadhirifu wa fedha, ambapo mwaka 2011, Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda aliagiza ufanyike uchunguzi, uliobaini kuwepo kwa madudu, hali iliyosababisha mzabuni aliyekuwepo kuondolewa.

Post a Comment

Previous Post Next Post