Amuua Mama yake kwa Panga akimtuhumu kuwa mchawi Makete Njombe

uzee
Na Edwin Moshi, Makete.
Jehi la polisi wilaya ya Makete mkoani Njombe linamshikilia Bw. Sadick Sanga (28) mkazi wa kijiji cha Unyangogo kata ya Iniho wilayani hapa, kwa tuhuma za kumuua kikatili Bibi Meluti Mbwilo (70) ambaye ni mama yake wa kambo
Tukio hilo limetokea Machi 14 mwaka huu ambapo mtuhumiwa alitenda mauaji hayo kwa kumkatakata na panga kichwani na miguuni wakati marehemu akiwa jikoni kwake
Akizungumzia tukio hilo Afisa upelelezi wilaya ya Makete ambaye pia ni kaimu OCD, Bw. Gosbert Komba amesema kuwa baada ya wananchi kugundua mauaji hayo, walimkamata mtuhumiwa na kisha wakatoa taarifa kwa jeshi hilo ambapo walifika mara moja na kumtia mbaroni mtuhumiwa
Amesema mtuhumiwa alikamatwa na kielelezo ambacho ni panga analodaiwa kulitumia kutekeleza mauaji hayo na kwa sasa anashikiliwa na jeshi hilo na atapandishwa mahakamani muda wowote kuanzia sasa kujibu mashitaka yanayomkabili
Bw. Komba amekiri vitendo vya mauaji ya kikatili kuendelea kushamiri wilayani Makete ambapo ametoa wito kwa wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani ni kinyume na sheria za nchi
Amesema mauaji hayo yanahusishwa na imani za kishirikina hivyo, kutokana na wazee wengi kuonekana wana macho mekundu hivyo watu kuwadhania kuwa ni wachawi hivyo kuwataka wananchi kuondokana na dhana hiyo potofu
“Unajua maeneo mengi hapa wilayani watu wanapikia kuni, na kuni zinatoa moshi, hawatumii gesi ama umeme huko vijijini, hivyo uwezekano wa watu kuwa na macho mekundu ni mkubwa kutokana na moshi unaotokana na kuni wakati wa kupika, haimaanishi macho mekundu yao eti ni wachawi” alisema Komba.

Post a Comment

أحدث أقدم