Na Maggid Mjengwa,
NIMEPATA kusimulia kisa cha kijana aliyehangaika sana kuusaka ukweli. Katika pitapita zake akaliona duka. Kibao kimeandikwa dukani; “Hapa tunauza ukweli”.
Kijana yule akauliza; “Mie nataka ukweli kilo nzima, mbona hujaandika bei?”
“Alaa, unataka kilo nzima ya ukweli?” aliuliza mwenye duka. “Naam” Akajibu kijana yule.
“Basi, zunguka uje ndani nikuambie bei yake”.
Alipoingia ndani dukani, kijana yule akaambiwa; “Kijana, hatukuandika bei, maana, gharama ya ukweli mzima ni uhai wako. Je, uko tayari kulipa?”
Kijana yule akatimua mbio. Nyuma aliacha vumbi. Hakuwa tayari kulipa gharama ya ukweli mzima.
Yumkini ukweli utakaousema mwanadamu waweza usiwafurahishe wachache, walakini, ukawa wenye kuleta tija, furaha na matumaini kwa walio wengi.
Mimi nitasena hapa ukweli wangu, kuwa Baraza jipya la mawaziri ni mabadiliko ya sura ya Baraza lakini si mabadiliko ya mfumo uliosababisha udhaifu wa kiutendaji ikiwamo ‘madudu’ yale tuliyoyaona bungeni hivi karibuni. Na kauli za baadhi ya mawaziri zinathibitisha hilo; wengi wameahidi kuanzia na yanayotokana na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ( CAG).
Hakika, tatizo letu kubwa ni la kimfumo. Unaanzia na tunavyompata Rais wa nchi, unakuja na tunavyowapata wabunge wetu, unaendelea na mawaziri wetu wanavyopatikana na hata baadaye watendaji wetu.
Katika nchi hii Rais ana wakati mgumu sana. Maana, mfumo unamtaka awachague mawaziri kutoka miongoni mwa wabunge wa chama chake. Si ajabu juzi hapa Rais amewateua wabunge wapya kutoka kwenye nafasi zake kumi na kuwafanya kuwa mawaziri hata kabla ya kuapishwa bungeni. Ilikuwa dhahiri, kuwa Rais aliwaona mawaziri wake wa kumsaidia miongoni mwa majina yale mapya ya wabunge aliowateua.
Kwa mantiki hiyo basi, mfumo ulio nafuu kwetu ni kumpa Rais uwezo wa kuchagua mawaziri nje ya Bunge. Kwamba Katiba ijayo iweke wazi kuwa mawaziri wasiwe wabunge kwa wakati mmoja. Kama Rais ataamua kumteua mbunge kuwa waziri, basi, mbunge huyo ajiuzulu kiti chake cha ubunge. Maana, mbunge ni mwakilishi wa wananchi ambaye moja ya majukumu yake bungeni ni kuisimamia Serikali. Mwanadamu huwezi kupanda farasi wawili kwa wakati mmoja.
Tuna tatizo jingine hatuliweki wazi lakini lipo na linakomaa; uteuzi wa Baraza la Mawaziri katika mfumo wetu wa sasa unaangalia pia jiografia ya nchi yetu. Inaangaliwa kama katika Baraza jipya Mbeya wamepata mawaziri? Dodoma? Mwanza….
Na tukitoka hapo tunakuja ni wangapi kwa kila mkoa? Ni mfumo mbaya unaozoeleka. Maana, mitaani watu wa Singida wanaweza kuhoji? Mbona sisi tumesahaulika kwenye Baraza jipya? Kana kwamba ni Baraza la mikoa wakati ni la taifa.
Kwa maelezo kamili ingia hapa:- http://www.kwanzajamii.com/?p=3854
Post a Comment