Jiji la Mwanza kuwaondoa wamachinga Makoroboi


 Jiji la Mwanza kuwaondoa wamachinga Makoroboi

Halmashauri  ya Jiji la Mwanza imesema kwamba inakusudia kuwahamisha wafanyabishara ndogondogo maarufu kama wamachinga wanaopanga na kuuza bidhaa zao katika eneo la Makoroboi ikiwa ni utekelezaji wa Sheria Ndogo ya Mipango Miji. 
  
Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Wilson Kabwe (pichani), amesema kuwa azma ya kuwaondoa wamachinga hao inatarajiwa kutekelezwa wakati wowote baada ya taratibu kukamilika. 
  
Alisema kuwa katika kutenga maeneo rasmi kwa ajili wamachinga kufanyia biashara zao, Kamati ya Mipango Miji, Ujenzi na Mazingira ya Halmashauri hiyo iliweka vigezo kwa ajili ya kuepusha muingiliano wa shughuli za kijamii na biashara. 



Kwa mujibu wa Kabwe, baadhi ya vigezo vilivyowekwa na Kamati hiyo ni kwamba maeneo yenye nyumba za ibada, shule pamoja na hospitali hayapaswi kutumiwa na wamachinga kwa biashara zao. 
  
Alibainisha kuwa eneo la Makoroboi, lina nyumba za ibada za Jumuiya ya Hindu na Swaminnarayan pamoja na shule ya watoto wadogo na kwamba ni wakati mwafaka kwa wamachinga kuanza kuhama wenyewe na kwenda maeneo waliyotengewa rasmi kwa ajili ya biashara zao. 
  
Aliyataja baadhi ya maeneo hayo ni barabara ya Liberty-Uhuru, Relini, Mwananchi, Kamanga, Kitangiri, Kiloleli na Mkuyuni. 


Habari na -  GEORGE RAMADHAN
SOURCE: NIPASHE

Post a Comment

أحدث أقدم