Boban kuwakosa Gambia Jumapili

Boban kuwakosa Gambia Jumapili

WACHEZAJI Nassoro Masoud ‘Cholo,’ Haruna Moshi ‘Boban’ na Waziri Salum wa timu ya soka ya Tanzania, Kili Taifa Stars, wataikosa mechi ya Jumapili dhidi ya Gambia kutokana na kuwa majeruhi na kufiwa.
Kwa mujibu wa daktari wa timu hiyo, Mwanandi Mwankemwa, Cholo anasumbuliwa na tatizo la goti ambalo kati ya leo au kesho, anatarajiwa kufanyiwa uchunguzi zaidi kujua ukubwa za tatizo.
Mwankemwa alisema Boban anasumbuliwa na nyama za paja na kusema, licha ya kuanza mazoezi, bado yuko chini ya uangalizi zaidi ili kuhakikisha hali yake inaimarika huku Salum akiikosa mechi hiyo kutokana na msiba wa baba yake uliotokea Mjini Zanzibar.
“Hadi sasa, Cholo tayari tumemuengua kwenye kikosi hicho kutokana na majeruhi aliyonayo na kama kipimo kitaonyesha ana tatizo, atafanyiwa upasuaji. Salum ameondoka tangu juzi kwenda Zanzibar, amefiwa na baba yake,” alisema Mwankemwa.
Alisema wachezaji wengine wako fiti na wanaendelea vizuri na mazoezi kwa ajili ya mechi hiyo kwani Nurdin Bakari aliyekuwa na tatizo la nyama za paja, Mwadin Ally ambaye aliumia kidole juzi pamoja na Thomas Ulimwengu na kusema kuwa nyota hao wako fiti.
Katika hatua nyingine, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura, alisema waamuzi kutoka Zimbabwe ndiyo watakaochezesha pambano hilo.
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), mwamuzi wa kati atakuwa Ruzive Ruzive. Waamuzi wasaidizi ni Salani Ncube na Edgar Rumeck huku mwamuzi wa akiba akiwa Norman Matemera.
Wambura alisema mbali na waamuzi hao, kamishna wa mechi hiyo atakuwa ni Fanie Wallace Mabuza kutoka Swaziland wakati mtathmini wa waamuzi, atakuwa ni Ali Baligeya Waiswa.
Alisema waamuzi hao watawasili nchini leo saa 1.20 usiku kwa ndege ya Kenya Airways huku Kamishna wa mechi hiyo atawasili saa 12.50 jioni kwa ndege ya South African Airways, huku mtathmini wa waamuzi atatua saa 7.55 mchana kwa ndege ya Kenya Airways.
Aidha Wambura alisema Gambia walitarajia kuwasili nchini jana saa 9.20 usiku kwa ndege ya Kenya Airways tayari kwa ajili ya mechi dhidi ya Taifa Stars, itakayopigwa Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Kikosi cha timu hiyo chenye wachezaji 22 wakiwemo tisa wanaocheza mpira wa kulipwa nje ya nchi hiyo kitafikia kwenye Hoteli ya Sapphire iliyoko Mtaa wa Lindi na Sikukuu eneo la Kariakoo.
Wachezaji walioko katika msafara huo ni Musa Camara, Abdou Jammeh, Momodou Futty Danso, Lamin Basmen Samateh, Ousman Koli, Pa Saikou Kujabi, Mustapha Kebba Jarju, Yankuba Mal Ceesay na Demba Savage.
Wengine ni Saihou Gassama, Alieu Darboe, Momodou Ceesay, Pa Modou Jagne, Tijan Jaiteh, Bubacarr Sanyang, Christopher Allen, Musa Yaffa, Sulayman Marr, Mamut Saine, Hamsa Barry, Ali Sowe, Omar Colley na Saloum Faal.
Aliongeza kuwa kikosi hicho cha Gambia kitaanza mazoezi leo katika Uwanja wa Taifa jioni na asubuhi katika dimba la Karume.

Post a Comment

أحدث أقدم