Polisi yafuta maandamano ya Waislamu

 Polisi yafuta maandamano ya Waislamu

JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limepiga marufuku maandamano ya Waislamu yenye lengo la kupinga Baraza la Mitihani la Taifa (Necta) kwa madai kuwa limewafelisha wanafunzi wa dini hiyo katika somo la elimu ya Uislamu.
Kaimu Kamishna wa Polisi wa kanda hiyo, Ahmed Msangi, alisema sababu za kusitisha maandamano hayo ni kutokana na jeshi hilo kutokuwa na idadi ya askari wa kutosha kutoa ulinzi kwa vile waumini hao watakuwa wakitokea katika misikiti mbalimbali.
Alisema kuwa waandamanaji walikuwa na lengo la kwenda katika Ofisi ya Wizara ya Elimu na Necta lakini tayari kamati ya maandalizi ilikutana na Waziri wa Elimu Dk. Shukuru Kawambwa pamoja na viongozi wengine wakafikia muafaka.
Wakati huohuo, Waziri Kawambwa, amewasihi waumini hao kusitisha maandamano kwa vile suala hilo amelishalitolea ufumbuzi.
“Nawasihi jamii, dini na Watanzania wajiepushe na maandamano kwani maelezo yameshatolewa kwa kina na viongozi wa pande zote zishakubaliana,” alisema.
Kwa mujibu wa Kawambwa dosari katika somo hilo, imetokana na kutumiwa kwa teknolojia mpya ambayo imekuwa ni mara ya kwanza kutumika katika masomo; teknolojia hiyo ilisababisha hitilafu kwa baadhi ya masomo ikiwemo la Kiislamu, kwani katika masomo yenye karatasi mbili ilitumika kwa usahihi wakati somo lenye zaidi ya karatasi hizo ilionyesha dosari.
Kawambwa aliongeza kuwa wizara itaunda kamati ya wataalumu kuiwezesha serikali kujiridhisha zaidi na hatua zilizochukuliwa na Necta ili dosari hiyo isijirudie.

Post a Comment

أحدث أقدم