Mechi yamzuia Maximo Brazil

KOCHA Marcio Maximo wa Brazil aliyekuwa awasili jana kwa mazungumzo ya kuinoa timu ya Yanga, ameshindwa kufanya hivyo kutokana na timu yake ya Democrata F.C ya Mjini Rio de Jeneiro, kukabiliwa na mechi muhimu.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, mechi hiyo muhimu itachezwa Jumamosi hii, hivyo ujio wa Maximo utakuwa baada ya kupita kwa mechi hiyo muhimu kwa timu hiyo.
“Yanga inapenda kuwajulisha juu ya ujio wa Kocha Marcio Maximo, aliyetarajiwa kuwasili leo (jana), sasa anatarajiwa kuwasili mwishoni mwa wiki hii.
“Maximo ambaye tayari amekwishatumiwa tiketi ya safari ya kuja, ameshindwa kuwasili leo (jana), kutokana na timu yake ya Democrata F.C ya mjini Rio de Janeiro, Brazil kukabiliwa na mechi ngumu Jumamosi ya wiki hii,” alisema.
Sendeu alisema, baada ya kuwasili nchini atafanya mazungumzo na uongozi wa Yanga, ikiwamo kusaini mkataba wa kuinoa timu hiyo kwa michuano ya Kombe la Kagame itakayofanyika mwezi ujao.
Kwa mujibu wa Sendeu, Maximo amewaahidi makubwa wapenzi na mashabiki wa Yanga kwani baada ya kubeba jukumu hilo, atafanya jitihada za kukiimarisha kikosi cha ushindi ikiwamo kutetea ubingwa wa Kombe la Kagame.
Kwa sasa timu yake ya Democrata FC inashiriki michuano maalumu ya majimbo ikilenga kusaka nyota wa kuichezea timu ya taifa ya Brazil, wenyeji wa fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014.
Sendeu alisema kati ya mambo yatakayopewa msisitizo mkubwa na Maximo ni uwekezaji kwenye soka ya vijana kwa lengo la kupata nyota wa kesho, pia kuimarisha nidhamu kwa wachezaji.
Baada ya kusaini mkataba wa kuinoa Yanga, mtihani wa kwanza kwake utakuwa kuiwezesha kutetea ubingwa wa Kombe la Kagame ambalo timu hiyo ililitwaa Julai 10, mwaka jana chini ya Kocha Sam Timbe wa Uganda.
Michuano ya Kombe la Kagame itafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Julai 23 hadi Agosti 5 ambapo Tanzania Bara itawakilishwa na timu tatu; Simba, Azam na Yanga.
Ujio wa Maximo unangojewa kwa hamu na wapenzi na mashabiki wa Yanga, wakiami miaka minne ambayo kocha huyo aliyoishi nchini akiinoa timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars kati ya 2006 hadi 2010, kutamsaidia akiwa Jangwani.

Post a Comment

أحدث أقدم