WAKATI kampeni za wagombea uongozi katika uchaguzi mdogo kwenye klabu
ya Yanga ikitarajiwa kuanza rasmi leo, kocha mpya wa timu hiyo Mbelgiji
Tom Saintfiet, anatarajiwa kuanza kazi leo.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, kabla ya kuanza kazi, mchana wa leo atasaini mkataba wa kuinoa timu hiyo.
Alisema mkataba huo utasainiwa baada ya mazungumzo ya kina baina ya
kocha huyo tangu alipowasili nchini juzi, kilichobaki ni kumwaga wino
ili kuanza kazi.
Aidha, katibu wa kamati ya uchaguzi wa Yanga, Francis Kaswahili,
alisema kuwa maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Julai 15, yanaendelea.
Alisema kampeni kwa wagombea uongozi, zitaanza leo hadi Julai 14, ikiwa ni siku moja
kabla ya uchaguzi huo utakaofanyika ukumbi wa Diamond Jubile, jijini Dar es Salaam.
Wagombea nafasi ya uenyekiti iliyoachwa na Lloyd Nchunga, ni Yusuf Manji, John Jembele, Edger Chibula na Sarah Ramadhan.
Wagombea nafasi ya Makamu, ni Ayoub Nyenze, Stanley Kevela ‘Yono’ na Clement Sanga.
Nafasi ya ujumbe inawaniwa na Abdallah Binkleb, Edger Fongo, Waziri Ahmed, Jumanne Mwammenywa, Beda Tindwa na Ramadhan Saidi.
Wengine ni Omary Ndula, Shaban Katwila, Ramadhan Mzimba, Lameck Nyambaya,
Peter Haule, Justine Baruti, Abdalah Mbaraka,
Yono, Moses Valentino, Aaron Nyanda,
George Manyama, Abdalah Sharia Ameir,
Jamal Kisongo na Gaudiusus Ishengoma.
Uchaguzi huo unafanyika kuziba nafasi sita zilizo wazi baada ya
wahusika watano kujiuzulu kwa sababu na wakati tofauti na mmoja
akifariki dunia.
Nchunga aliyeingia madarakani Julai 18, 2010 kurithi kiti cha Imani
Madega, alijiuzulu Mei 23, 2012 kutokana na presha ya wanachama
إرسال تعليق