AKUFFO AZIDI KUTISHA, NGASSA AFUNGUA AKAUNTI YA MABAO MSIMBAZI

  AKUFFO AZIDI KUTISHA, NGASSA AFUNGUA AKAUNTI YA MABAO MSIMBAZI


Akuffo akishangilia bao dhidi ya Mathare Jumapili. Leo amefunga tena.
SIMBA imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 jioni hii kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha dhidi ya wenyeji JKT Oljoro katika mchezo wa kirafiki wa kujipima nguvu kabla ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, inayotarajiwa kuanza katikati ya mwezi ujao.
Mshambuliaji kutoka Stella Abidjan ya Ivory Coast, Mghana Daniel Akuffo ameendelea kutunisha akaunti yake ya mabao Msimbazi, akifikisha mawili wakati Mrisho Khalfan Ngassa amefungua rasmi akaunti yake ya mabao leo katika mchezo huo.
Akuffo aliifungia bao la kwanza Simba SC dakika ya 25, akiunganisha pasi ya Ngassa- hilo likiwa bao lake la pili tangu aanze kuichezea timu hiyo mwezi huu, baada ya awali kufunga kwenye Uwanja huo huo Jumapili dhidi ya Mathare United ya Kenya katika ushindi kama wa leo, 2-1.
Ngassa alifungua akaunti yake ya mabao Simba SC dakika ya 76 akiunganisha pasi ya Abdallah Juma ‘Dullah Mabao’ na Oljoro ilipata bao la kufutia machozi dakika ya 89 kwa penalti iliyotiwa nyavuni na Markus Mpangala baada ya Paschal Ochieng kumuangusha mchezaji huyo wa timu ya Maafande wa Jeshi la Kujenga Taifa kwenye eneo la hatari.    
Simba itakuwa na mechi nyingine ya kujipima nguvu Jumapili, Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam dhidi ya Coastal Union ya Tanga, kabla ya kumenyana na Azam katika mechi ya Ngao ya Jamii Septemba 8, mwaka huu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Post a Comment

أحدث أقدم