MOTO WAITEKETEZA MTWARA, Nyumba ya Waziri wa TAMISEMI Hawa Ghasia yachomwa moto, Jengo la Mahakama laendelea kuteketea.


Diwani Chehako nyumbani kwake
Diwani Chehako akiwa nyumbani kwake
POLISI leo wamelazimika kupiga mabomu ya machozi kutwa nzima katika kata ya Chikongola, Manispaa ya Mtwara Mikindani kutawanya wananchi walioizingira nyumba ya diwani wa kata hiyo Mohamedi Chehako kwa madai ya kuwahifadhi wachawi ndani ya nyumba yake, huku mwandishi wa habari mmoja akiripotiwa kujeruhiwa.

Habari ambazo hazijathibitishwa na kamanda wa polisi mkoani hapa, Maria Nzuki zinadai kuwa majira ya saa 10 kasoro za jioni watu wanaodaiwa kuwa ni wanajeshi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) waliingilia kati na kuanza kutembeza mkong’oto kwa wananchi ili kuzima vuguvugu hilo.

Mwandishi wa habari hizi alipojaribu kuwasiliana na kamanda Nzuki kwa njia ya simu za mkononi hakuweza kupatikana.

Wananchi walitoa tuhuma hizo baada ya kukuta ungo ikiwa na tunguri ndani yake ambayo inadaiwa kuwa ni ndege ya wachawi uwanjani kwake maeneo ya makabuli Msafa.

Wananchi walijikusanya nyumbani kwa diwani huyo na kumshinikiza awatoe wachawi nje ili waweze kuwadhibu, amri iliyopingwa na diwani huyo.

Kadri mda ulivyokwenda ndivyo wananchi walivyozidi kuongezeka na hatimaye kulijitokeza kundi la watu walioanza kutia vurugu, hali iliyomlazimu Chehako kuomba msaada wa polisi.

Mashuhuda wa tukio walimweleza mwandishi wa habari hizi kuwa polisi walipofika waliwasihi wananchi kutawanyika kwa kuwa ungo na tunguri zake zilikuwa zimeteketezwa kwa moto na diwani huyo mbele ya wananchi hao.

“Wananchi waliendelea kupinga na kudai ndani ya nyumba kuna rubani na abiria wa ndege nimewahifadhi…polisi wakawachagua wananchi watano na kuingia ndani ya nyumba kuwasaka watu hao…hawakuona kitu, walitoka nje na kuwamabia wenzao hata hivyo wenzao walibisha” alisema Chehako alihojiwa nyumbani kwake.

Aliongeza kuwa “walianza kurusha mawe nyumba…polisi walianza kupambana nao kwa kuwarushia mabomu…hata hivyo wananchi walikuwa wanakimbia na kwenda upande wapili kufanya vurugu”

Akihadithia mkasa huo, Chehako alibainisha kuwa ni kawada yake kuamka alfajiri kwa ajili ya sala ya asubuhi, lakini asubuhi ya jana alishindwa kuamka mapema, hata hivyo hakuweza kuhisi jambo lolote.

“Ilipofika saa 12 asubuhi nikaanza kusikia watu wakishangaa kitu nje, nilipotoka nikakuta nyungo na tunguri ndani yake…mara wakaja vijana wawili na pikipiki wakachukua ule ungo na kukimbia nao…nikawatuma vijana wawafuate waurudishe…walifanikiwa na nyungo ile ilirejeshwa nyumbani hapa na ndipo nilipouteketeza kwa moto” alisema na kuongeza kuwa “Nilidhani yatakuwa yameisha, lakini wananchi waliendelea kudai nimewafungia wahuska ndani, si kweli hakuna mtu humu ndani wala mimi sijui kilichotokea hadi hivyo vitu vikawa humu ndani”

Katika mapambano hayo ya wananchi na polisi, wananchi kwa kutumia mawe wamemjeruhi Mwandishi wa Habari wa Channel Ten mkoani hapa, John Kasembe kwa jiwe kichwani, sehemu za kisogoni ambapo ametibiwa zahanati ya Fajima na anaendelea vizuri.
Kwa mujibu wa Kasembe alipigwa mawe kichwani akiwa kazini kukusanya habari na wananchi waliokuwa wakiwarushia mawe polisi.

Ofisa wa polisi ambaye jina lake hakutaka litajwe kwa sababu si msemaji wa jeshi hilo amethibitisha kutokea kwa tuki hilo na kuongeza kuwa gari moja ya polisi PT 1421 limevunjwa kioo cha mbele kwa mawe.

Hadi saa 10.00 jioni bado polisi walikuwa wanaendelea kupiga mabomu ya machozi hewani huku wananchi wakionekana kujipanga katika makundi hali iliyotishia usalama wa maeneo hayo.

Angalia picha zaidi hapa chini
mwandishi wa Channel Ten, John Kasembe
mwandishi wa Channel Ten, John Kasembe

1
3
2
Habari na picha kwa hisani ya http://kusini.wordpress.com

Post a Comment

أحدث أقدم