Serikali ya Somalia kufanya mfumo wa mishahara kuwa wa kisasa

Mfumo mpya katika mwezi wa Aprili utaanza kutumiwa kuwalipa waajiriwa wa serikali, ikiwa ni pamoja na wajumbe hawa wa Kikosi cha Polisi ya Somalia, moja kwa moja kupitia Benki Kuu ya Somalia. [Na AFP Photo/AU-UN IST Photo/Stuart Price]
Na Adnan Hussein, Mogadishu

Serikali ya Somalia itaanzisha mpango mpya hapo Aprili wa kuwalipa waajiriwa wake kupitia mfumo wa automatiki unaodhibitiwa na Benki Kuu ya Somalia.


Waziri wa Fedha na Mipango Mohamud Hassan Suleiman aliiambia Sabahi kuwa programu hiyo ni moja miongoni mwa mipango kadhaa yenye lengo la kuufanya mfumo wa fedha nchini kuwa wa kisasa, kutoa uwiano wa bajeti na kuzuia ufisadi wa kitawala na kifedha.

Waajiriwa wa serikali kwa sasa wanalipwa fedha taslimu na wahasibu waliopangiwa katika wizara zao husika baada ya fedha kulipwa na Benki Kuu. Wahasibu ndio wenye dhamana ya kukusanya fedah na kumlipa kila mwajiriwa baada ya kutia saini risiti ya karatasi kama njia ya uthibitisho.

Mchakato huu, ambao unahusisha kutoa na kusafirisha kiwango kikubwa cha fedha na kujaza fomu za karatasi, mara nyingi hupelekea kuchelewa kwa mishahara na kupotea kwa fedha, Suleiman alisema.

Waziri alisema kuwa mfumo huo mpya utazuia kuchelewa huko na kupelekea uwajibikaji mzuri zaidi na uwazi katika udhibiti wa fedha za umma.

Kukiwa na mfumo wa malipo ambao ni automatiki, kila mwajiriwa wa umma atapewa akaunti yake binafsi katika Benki Kuu ambako mishahara yao itakuwa inawekwa kwenye akaunti hizo na kupatikana kwa kutumia kadi ya beki mwanzoni mwa kila mwezi.



Serikali pia inapanga kutoza kodi katika kampuni zinazotoa pesa taslimu, kampuni za mawasiliano ya simu, mirungi, sigara, na kwa wauzaji kwenye masoko ya maeneo, alisema. Kodi zitatozwa pia kwa bidhaa zinazoingia kupitia bandari za Mogadishu, Kismayo, Bosaso na Berbera.

"Tutapambana na ufisadi wa kiutawala na kifedha na tutaanzisha mipango ambayo itaturuhusu kukiusanya kodi zaidi na kutimiza ahadi zetu za kuwatumikia watu wa Somalia," Suleiman aliiambia Sabahi.

Shirika la Transparency International, asasi ya kiraia ya kimataifa inayopambana na ufisadi, ilizipa daraja Somalia, Afghanistani na Korea ya Kaskazini kuwa ndizo nchi fisadi zaidi miongoni mwa nchi 176 katika orodha yake ya 2012.

Msukosuko wa hali ya soko
Serikali lazima ichukue hatua zaidi za kudhibiti fedha za umma katika juhudi zake za kutuliza uchumi, wachambuzi waliiambia Sabahi.

Mwanauchumi Bashir Mardadi Salah alisema kuwa sheria lazima ziwekwe ili kuhakikisha kuwa mishahara ya watumishi wa umma inalipwa kwa shilingi ya Somalia ili kuimarisha thamani yake dhidi ya sarafu za kigeni. Hivi sasa, akiba ya fedha za kigeni katika Benki Kuu inakadiriwa kufikia dola milioni 17 na inapungua kwa kiwango cha kutisha, aliiambia Sabahi.

Salah alisema kuwa serikali inapaswa kuhifadhi fedha yoyote ya kigeni iliyo nayo ili kujenga akiba yake ili kuleta mzunguko mwingi wa shilingi ya Somalia ambazo zilipangwa kuchapishwa wakati wa serikali ya mpito lakini bado hazijatolewa.

Mwanauchumi Hiba Abdi Khalif alisema kuwa kuimarisha nafasi ya Benki Kuu pia itasaidia kusitisha ghiliba katika ubadilishaji wa fedha za kigeni na wafanyabiashara huru ambao hawawekewi sheria.

Ingawa Benki Kuu ya Somalia ilifunguliwa upya mwaka 2009, wafanyabiashara huru ndio wanaodhibiti viwango vya ubadilishaji fedha na wanaweza kulighilibu soko. Kwa miaka mingi, alisema, wafanyabiashara wamekuwa wakitumia fursa ya msukosuko wa uchumi ulioanzishwa na kukosena kwa sheria na upungufu wa shilingi ya Somalia iliyopo kwa ajili ya mzunguko na kughilibu viwango vya ubadilishaji fedha kwa kujipendelea wao.

Khalif alitahadharisha dhidi ya kushindwa kwa Wizara ya Fedha na Mipango kuwakamata watu waliohusika na kughilibu viwango vya ubadilishaji fedha, ambacho kimeathiri familia za Wasomali wengi ambazo zinategemea fedha kutoka nje.

Hapo tarehe 17 Januari, Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamud alimteua mwanauchumi Abdisalam Omer kuwa gavana mpya wa Benki Kuu ya Somalia. Omer amefanya kazi katika Benki ya Dunia na ana digirii za uzamifu katika utawala wa umma kutoka Chuo Kikuu cha Tennessee, Marekani.

Post a Comment

أحدث أقدم