Newzz:- SHEKHE PONDA ADAIWA KUUAWA KWA RISASI MOROGORO...

Shekhe Ponda Issa Ponda.
Habari zilizopatikana muda mfupi uliopita zinadai kwamba Mhubiri mashuhuri wa dini ya Kiislamu nchini, Shekhe Ponda Issa Ponda amepigwa risasi mjini Morogoro mapema leo.
Kwa mujibu wa walioshuhudia tukio hilo, wanadai kwamba Shekhe Ponda alipigwa risasi na kujeruhiwa vibaya begani wakati akishuka kutoka teksi iliyompeleka kwenye eneo la Uwanja wa Ndege kuendesha mhadhara wa Sikukuu ya Iddi El Fitri.
Mashuhuda hao waliendelea kudai kwamba, chanzo cha tukio hilo ni polisi waliofika eneo hilo kwa nia ya kumkamata Shekhe Ponda, na ndipo umati wa watu wanaoaminika kuwa ni waumini wa dini ya Kiislamu walipowavamia na kuibuka vurugu kubwa.
Katika kudhibiti hali hiyo, inadaiwa polisi hao walilazimika kutumia risasi za moto ndipo kwa bahati mbaya ikampata Shekhe Ponda ambaye anasemekana alikuwa katika harakati za kuwatuliza waumini hao.
Lakini chanzo kingine ambacho hakikupenda kutaja jina kilifika mbali na kudai kushuhudia mwili wa Shekhe huyo ukipakiwa kwenye gari ambalo hatahivyo hakulitaja na kuondoshwa eneo la tukio.
"Ni kweli nimemuona Ponda akichuruzika damu nyingi begani huku dalili zote zikionesha kwamba amefariki dunia," kiliongezea chanzo hicho.
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Faustine Shilogile, alikana kupata taarifa hizo za kifo cha Shekhe Ponda na kusema kwamba mengi yanazungumzwa kuhusiana na hilo.
Kamanda huyo aliongeza kwa kusema kwamba kama kuna ukweli katika hilo basi yeyote mwenye taarifa za uhakika kuwasiliana na polisi haraka iwezekanavyo.
Mpaka tunarusha habari hii kumeendelea kuwapo kwa taarifa za kutatanisha kuhusiana na madai ya kifo cha Shekhe Ponda ingawa taarifa zote zinathibitisha uwepo wake mkoani humo.

Post a Comment

Previous Post Next Post