Wachezaji Simba waletewa bonge la fundi

AFRIKA Mashariki ukitafuta ni kocha yupi anasifika kwa mipango uwanjani kama ilivyo kwa Jose Mourinho wa Chelsea ya Uingereza utatajiwa jina la Sredojevic Milutin ‘Micho’ wa Uganda na Zdravko Logarusic wa Simba.
Logarusic sasa ameanza mipango yake ya msimu ujao anakotaka kurudisha heshima ya klabu hiyo, ametaka kuajiriwa kwa mtaalamu mmoja anayeitwa Mikael Igendia spesho kwa wachezaji wake.
Unajua kwa nini? Logarusic raia wa Croatia ameitumikia Simba kwa miezi sita na baadaye akagundua jambo moja kubwa kwamba shida moja iliyokisumbua kikosi chake ni kutokana na kuona wachezaji wake wakikosa mazoezi mazuri ya kisasa ya viungo.
Kulimaliza tatizo hilo tayari ameshaliweka katika ripoti yake aliyoikabidhi kwa Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga, kocha huyo ametaka klabu hiyo kufanya maboresho katika benchi lake la ufundi kuajiriwa kwa Igendia ambaye ni maalumu kwa kazi hiyo.
Igendia ambaye ni raia wa Kenya aliwahi kufanya kazi na Logarusic wakiwa Gor Mahia ya Kenya ambapo kutokana na kuyajua majukumu yake hayo, kocha huyo ametaka Simba imuwahi haraka mtaalamu huyo aweze kutua Simba msimu ujao ambao amesema utakuwa na mapambano ya kweli.
Akizungumza na Mwanaspoti, Logarusic alisema Simba ikimaliza kumleta Igendia itakuwa imepunguza majukumu kwa makocha wa kikosi hicho ambapo mtalaamu huyo atakuwa na kazi ya kuwaweka sawa wachezaji wao kimwili kabla ya kuanza kupokea mbinu mbalimbali.
Logarusic alisema kwa sasa Igendia anamalizia mafunzo maalumu nchini Norway ambapo ameitaka Simba kuhakikisha inaanza mawasiliano naye haraka muda wowote akigusa ardhi ya Kenya.
“Nataka huyo mtu aje (Igendia) namjua vizuri hasa uwezo wa kazi yake, tumekuwa tukipata shida hasa katika kuwandaa wachezaji, nataka kuona kila kitu kinafanyika kitaalamu msimu ujao, tukimpata Igendia tutakuwa tumefanya jambo zuri,” alisema Logarusic.
Akimzungumzia Igendia, Katibu Mkuu wa Gor Mahia, George Bwana alisema anamjua vizuri Igendia ambaye ana asili ya Finland ambapo amesema mtalaamu huyo ni kati ya watu wazuri wanaoweza kuwandaa wachezaji ambaye kwa sasa amemaliza mafunzo yake na anatafuta kazi ya kufanya.
“Hatukuwa na mkataba na Igendia alivyokuwa hapa Gor (Mahia), kama Logarusic akimpata nafikiri atakuwa amefanya kitu kizuri kwa timu yake ni kijana mdogo anayejua kuwatengeneza wachezaji, alipokuwa hapa alitufanyia kazi nzuri sana, nimezungumza naye hivi karibuni ameniambia amemaliza mafunzo na sasa anatafuta kazi ya kufanya, waambie Simba wamuwahi haraka,” alisema Bwana.
 Chanzo:- Mwanaspoti

Post a Comment

أحدث أقدم