Yanga wazuiwa kusajili mastaa wa nje ya nchi


 
Mholanzi, Hans van Der Pluijm.

KAMATI ya usajili ya Yanga kwa sasa imesimama kutafuta wala kufanya usajili wa wachezaji wa kigeni kutokana na kuamua kufuata maagizo ya aliyekuwa kocha mkuu wa timu hiyo, Mholanzi, Hans van Der Pluijm.
Hatua ya kusimama kufanya usajili huo, inakuja baada ya viongozi wa Yanga kutii na kuheshimu kauli iliyotolewa na Pluijm kuwa atawaletea kifaa kitakachokuwa msaada, hivyo maamuzi yote juu ya usajili wa mchezaji wa nje yanasubiri jina litakalotumwa na kocha huyo.
Tayari Mholanzi huyo yupo Ghana kwa ajili ya zoezi hilo na akishamaliza shughuli hiyo, anatarajia kujiunga na Al Shoala mara moja kwa ajili ya kuanza kazi.
Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu, amesema kwamba kwa sasa Yanga imetulia kuhusu usajili wa nje na sababu kubwa ni kutimiza ahadi hiyo kwani wanasubiri tamko la kocha huyo wa zamani wa Berekum Chelsea ya Ghana.
Hata hivyo, Njovu alifafanua kwamba si lazima kocha huyo atafute mchezaji kutoka kwenye Ligi Kuu ya Ghana au awe raia wa Ghana, isipokuwa amekwenda huko kwa kuwa kuna ‘connection’ nyingi.
“Wakati anaondoka kwa ajili ya kwenda kufanya shughuli hiyo, alituambia kwamba ameshakisoma kikosi vizuri ndani ya miezi sita, kwa hiyo anajua amlete mchezaji wa aina gani ili kikosi kiwe bora zaidi msimu ujao, ndiyo maana tunamsubiri yeye kuhusu usajili wa nje.
“Lakini hata kama yupo Ghana haimaanishi kwamba ni lazima ataleta mchezaji wa Ghana, anaweza kusajili wengine ila anaamini akiwa hapo anaweza kuwapata na wengine wa nchi nyingine kutokana na uzoefu wake,” alisema Njovu na kuongeza:
“Unajua mchezaji wa nje anayetakiwa hapa ni mmoja tu kwa ajili ya kukamilisha hesabu za wachezaji watano, tayari tunaye Haruna Niyonzima, Mbuyu (Twite), Okwi (Emmanuel) na Kiiza (Hamis), kwa hiyo anasubiriwa huyo tu, tufunge masuala ya usajili wa huko nje.”
Imeelezwa kuwa, Pluijm anaweza kumpotezea kiungo wa Ghana, Joseph Zuttah, aliyekuwa na malengo naye ya kumleta Jangwani tangu awali, baada ya kupewa taarifa kwamba kwa sasa ni mtovu wa nidhamu.

Post a Comment

أحدث أقدم