Shangazi ya marehemu, Evelyne Komba amebainisha kuwa maamuzi hayo yalifikiwa juzi baada ya kuusindikiza mwili wa marehumu ili uhifadhiwe katika chumba cha maiti katika Hospitali ya Wilaya ya Mpanda, chini ya ulinzi mkali wa Jeshi la Polisi kupitia Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU).
Aliongeza kuwa vurugu zilizotokea makaburini kwa ndugu wa baba mzazi wa marehemu kucharazwa fimbo na kudungwa 'mangumi' baada ya familia ya mama wa marehemu kufukia kaburi lililochimbwa na familia ya baba mzazi wa marehemu ndio kulikochochea uhasama mkubwa baina yao.
Shangazi huyo wa marehemu alisema ndipo walipolazimika kuita Polisi ambao waliweka ulinzi mkali nyumbani kwa bibi ya marehemu mtaa wa Kawajense Madukani, ukifanyiwa tarartibu za maziko na kuamuru mwili huo kurejeshwa katika chumba cha maiti hospitalini.
"Mwili huo hatimae ulichukuliwa na 'defender' (gari la polisi) la Polisi nyumbani kwetu nasi upande wa familia ya baba wa marehemu tulipanda gari hilo na kuusindikiza mwili huo mpaka uliohifadhiwa mochwari. Ndipo hapo hapo tulipokutana na kufikia maamuzi hayo," alisema Evelyne.
Hata hivyo alikiri kuwa wao familia ya baba wa marehemu wote walizira kuhudhuria maziko ya mtoto huyo wakihofia usalama wa maisha yao.
"Hatukuweza kuhudhuria maziko ya mtoto Junior kwa sababu bado kuna uhasama mkubwa baina ya familia hizi mbili sasa kule kuna vifaa vya kuchimbia kaburi vikiwemo sepetu, majembe vingeweza kutumika na wenzetu kutudhuru.Tuliona tuepushe dhahama hiyo kwa kutokwenda kuhudhuria maziko ya mtoto huyo," alisema kwa hisia kali .
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, baba wa marehemu Joseph Bacho (26), alikiri kuwa amejisikia huzuni kubwa kwa kukosa kuhudhuria maziko ya mwanae Junior akidai anafikiria kuwachulia hatua zaidi za kisheria hata hivyo hakuzifafanua.
"Najisikia huzuni kubwa nilihofia usalama wa maisha yangu, hivyo sikuweza kuhudhuria maziko ya mwanangu Junior. Ujue uhasama wa wakwe zangu uliibuka baada ya Junior kufariki dunia, wakidai eti hawanitambui kama baba yake mzazi marehemu kwa sababu zijatoa posa. Sasa kwa nini wadai baada ya mtoto kufikwa na umauti badala ya kunidai akiwa bado yu hai?" anahoji Joseph .
Baadhi ya wanandugu waliohojiwa na mwandishi, kwa masharti ya
kutoandikiwa wamekiri kuwa familia ya mama mzazi wa marehemu iliuchukua mwili huo saa nane mchana, katika chumba cha kuhifadhia maiti hospitalini hapo na kuustiri saa 12 jioni jana.
Familia hizo mbili zote zikiishi mtaa mmoja wa Kawajense Madukani, mjini hapa, zilijikuta zikiingia katika uhasama mkubwa hivi kiasi cha kupigana fimbo na ngumi makaburini katika ugomvi wa kugombea kuzika mwili wa mtoto Junior Bacho.
Sababu kubwa ya mpasuko huo imeelezwa kuwa ni mahari, kwani wazazi upande wa mama wa mtoto huyo walikuja juu na kumzuia baba wa mtoto, Joseph Bacho asishiriki katika shughuli zozote za maziko ya mtoto wake wakidai hawamtambui kwa kuwa hajatoa mahari kwa binti yao.
Inaelezwa kuwa, Joseph na mzazi mwenzake, Anna Kizo (20) walimzaa mtoto Junior Bacho nje ya ndoa, ambapo hadi umauti unamfika mtoto huyo, baba yake mzazi alikuwa hajajitambulisha kwa upande wa mwanamke wala kutoa mahari.
Na kwamba, tangu kuzaliwa kwa mtoto huyo, alikuwa akiishi na kulelewa na mama yake mzazi, Anna nyumbani kwa wazazi wake.
Kwa mujibu wa mashuhuda vurugu hizo ziliibuka baada ya upande wa ndugu wa baba wa mtoto kuweka msiba nyumbani kwao na kuandaa taratibu za kumzika mtoto huyo.
Hata hivyo, kitendo hicho kilipingwa na upande wa mama wa mtoto, ukisema ndio wenye haki ya kumzika mtoto huyo ambaye hawakuwahi kumtambua kisheria baba yake mzazi.
Ndugu wa upande wa baba ulifanikiwa kuchimba kaburi, kuutoa mwili mochari na kuufikisha nyumbani tayari kwa maziko, lakini vurugu za upande wa pili ikiwa pamoja na ndugu upande wa mama kufukia kaburi, zilisimamisha shughuli zote, huku malumbano yakishika hatamu hadi askari wa jeshi la polisi kupitia Kikosi chake cha Kuzuia Fujo (FFU) kilipolazimika kuingilia kati na kusimamia shughuli na kuurudisha mwili katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Wilaya ya Mpanda.
Inaelezwa kitendo cha upande wa mama wa mtoto kufukia kaburi ndiko kulikochangia kuchochea vurugu hadi FFU walipoingia kati.
Ilivyoanza Mkasa mzima unadaiwa kutokea mtaani hapo Alhamisi wiki iliyopita, siku ambayo mtoto huyo alifariki dunia katika Hospitali ya Wilaya ya Mpanda alikokuwa akiuguzwa na shangazi yake, Evelyne Komba na bibi yake mzaa baba, Teddy Francis.
Inaelezwa kuwa, wakiamini wana haki zote za kumzika mtoto huyo, waliuchukua mwili na kuweka msibani nyumbani kwao, jambo lililopingwa na upande wa mama wa mtoto waliokuja juu na kusema hawamtambui baba wa mtoto kwa kuwa hakuwa ametoa mahari.
Inadaiwa Joseph aliamua kumchukua mwanae huyo Juni 18 , mwaka huu kwa nguvu kutoka kwa mama yake mzazi na kumpeleka hospitalini alikolazwa kwa matibabu baada ya kubainika kuwa anasumbuliwa na utapia mlo mkali .
Kwa mujibu wa mashuhuda ndipo upande wa ndugu wa mama mzazi wa marehemu walipozira ikidaiwa kuwa hawakuweza kufika hata siku moja kumjulia hali mtoto huyo aliyekuwa akiuguzwa hospitalini hapo na shangazi yake Evelyne na bibi yake Teddy hadi umauti ulipomfika .
Licha ya upande wa ndugu wa mama mzazi wa marehemu kushushiwa tuhuma na lawama hizo nzito waliendelea na msimamo wao kwamba walikuwa na haki ya kumzika marehemu hivyo nao wakaamua kuweka msiba nyumbani kwa mama wa marehemu katika.
Ndipo , Juni 27 wazee wa Mtaa wa Kawajense waamua kuingilia kati mgogoro huo kwa kuzikutanisha pande hizo mbili zilizokuwa zikivutana na kufikia uamuzi kuwa msiba uwe nyumbani kwa baba wa marehemu.
Kufutia uamuzi huo shangazi wa marehemu aliongoza ndugu zake akiwemo baba mzazi wa marehemu hadi chumba cha kuhifadhi maiti katika Hospitali ya wilaya ya Mpanda mjini hapa na kuuchukua mwili wa marehemu kisha kuupeleka nyumbani kwa bibi ya marehemu kwa ajili ya maandalizi ya maziko yake.
Maziko ya mtoto huyo yalipangwa kufanyika katika makaburi ya Kawajense ÐMsufini, ambako upande wa ndugu wa baba mzazi wa marehemu walichimba kaburi katika eneo hilo, lakini muda mfupi baada ya kukamilisha kuchimba kaburi hilo ndugu wanaodaiwa wa upande wa mama mzazi wa marehemu waliwawavamia wachimba kaburi na kuwalazimisha kulifukia .
Waombolezaji waliokuwa msibani nyumbani kwa bibi ya marehemu baada ya kutaarifiwa tukio hilo,lililotokea makaburini walitimua mbio na kuelekea makaburini na kukuta baadhi ya wanandugu upande wa mama wakimalizia kufukia kaburi hilo.
Walipoulizwa sababu za kufukia kaburi hilo, walianza kufoka ndipo inadaiwa kundi la ndugu wa mama wa marehemu waliibuka na kuanza kuwashambulia kwa kuwacharaza fimbo ndugu wa baba mzazi wa marehemu .
Post a Comment