Makundi ya urais yatawala mjadala wa Escrow bungeni

Dodoma. Makundi ya urais ndani ya CCM ni miongoni mwa mambo ambayo yameuteka mjadala wa Akaunti ya Escrow katika Bunge.
Tangu kuanza kwa mjadala wa Akaunti ya Escrow Jumatano iliyopita kumekuwa na sintofahamu iliyotokana na baadhi ya wabunge wa CCM kujikita katika kuangalia urais zaidi.
Hali hiyo ilifanya kupunguza ushiriki mzuri wa baadhi ya wabunge kuhofia kuingizwa kwenye chuki ya makundi ya urais kupitia mjadala huo.
Baadhi yao walisikika wakishutumu hatua ya uchotaji wa fedha hizo, kiasi cha Sh321 bilioni katika makundi madogo madogo nje ya Ukumbi wa Bunge, lakini hawakuonekana wakichangia ndani ya Bunge.
Hata hivyo, hatua ya vyama kupewa jukumu la kupeleka majina ya wachangiaji katika ofisi ya Katibu wa Bunge, nayo inaonekana kuwanyima fursa baadhi ya wabunge kuchangia katika mjadala huo.
Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimroad Mkono ni mmoja wa waathirika wa utaratibu huo, ambapo alilalamika bungeni kuhusu kutopewa nafasi ya kuchangia.
Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Azzan Zungu alimwambia aende kwenye chama chake akazungumze nao maana wao ndiyo walioleta majina ya wachangiaji.
“Mimi niliomba kuchangia, lakini nikapewa masharti kama ninataka kuipata nafasi hii niwasaidie (Serikali),” alisema mbunge mwingine wa CCM ambaye hakutaka jina lake litajwe.
Makundi ya urais
Shinikizo la kutaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kujiuzulu katika nafasi hiyo linatajwa kuwa ni miongoni mwa mambo yanayotajwa kuwa ni mbinu za kumchafua ili mbio zake za kusaka urais ziingie dosari.
Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira alisema kama kuna watu ambao wanataka urais kwa kuchafuana, hawafai kushika nafasi hiyo.
Mbinu hizo chafu zinatajwa kufanywa na wabunge walio ndani ya chama chake ambao wanatajwa kuyaunga mkono makundi mengine.Hofu hizi za makundi ya urais, yameufanya mdahalo huo kwa upande wa CCM kujikita katika kuhakikisha kuwa kila mmoja anajilinda ili asilichafue kundi alilomo.
- Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم