Maziwa yatia hofu wamama


BAADHI ya akinamama wanaowanywesha watoto wao maziwa aina ya Lactojen1, wameingiwa na hofu kutokana na maziwa hayo kuadimika sokoni.
Wakizungumza na Tanzania Daima Jumapili kwa nyakati tofauti, akina mama hao walisema kuwa hivi sasa maziwa hayo yamekuwa bidhaa adimu kupatikana kutokana na wauzaji wengi kutokuwa nayo.
Jacquline John alisema kuwa mtoto wake wa miezi mitano sasa amekuwa akinywa maziwa hayo kutokana na yeye kuwa kazini lakini kwa anashindwa la kufanya kwa kuwa kwa miezi miwili hayapatikani.
“Mimi nilimwanzisha mwanangu Lactogen I, hayajawahi kumletea madhara yoyote lakini hivi sasa nachanganyikiwa kwani hayapatikani hata uzunguke maduka yote katika maeneo ninayoishi ya Tabata,” alisema.
Naye Gracey Gibson, alisema kuwa amepata woga wa kumuanzishia mwanae maziwa mengine kutokana na hofu ya kuweza kumletea madhara ikiwemo kuharisha au kuishiwa maji mwilini.
Alisema kuwa wapo wanaompa ushauri wa kumtaka amwanzishie maziwa ya ng’ombe lakini baadhi ya wataalam wamekuwa wakitoa angalizo juu ya maziwa hayo hasa kutokana na kuwa na protini nyingi na yanaweza kuchangia mtoto kupata pumu.
“Hivi kama kuna shida juu ya maziwa ya Lactojen 1, si bora Serikali itujulishe maana haiwezekani wauzaji wote washindwe kuwa nayo bidhaa hiyo,” alisema.
Mmoja wa wauzaji wa rejareja, Salum Issa alisema kuwa amejitaidi kutafuta maziwa hayo kwa takribani mwezi mmoja sasa lakini hajaweza kupata. “Mimi nina wateja wengi wanaotumia bidhaa hiyo, nimejaribu kuzunguka kuanzia kule wanakouza jumla lakini kote huko unaelezwa maziwa hayo hakuna kwa sasa,” alisema.
Dk. Namala Mkopi, alisema kuwa iwapo maziwa hayo hayapatikani sokoni wazazi wanaofanya kazi wanaweza kuwaanzishia watoto wao maziwa mengine ili kuhakikisha wanapata maziwa wakati wakiwa hawapo karibu nao.
“Mara nyingi kama kuna upungufu wa maziwa unaweza kumuanzisha maziwa mengine, tunaamini kuwa hakuna madhara yanayoweza kuwapata ikiwa vyombo anavyotumia vinaandaliwa katika mazingira mazuri,”alisema.
Via- Tanzania Daima

Post a Comment

أحدث أقدم