Mkombozi Benki: Hatuhusiki kutakatisha fedha

Dar es Salaam. Benki ya Biashara ya Mkombozi imesema, haihusiki na utakatishaji fedha zilizoibiwa katika Akaunti ya Tegeta Escrow Sh306 bilioni.
Kauli ya Benki ya Mkombozi inakuja wakati Ripoti ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) kuitaka Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuitangaza benki hiyo kama benki ya utakatishaji fedha nchini.
Taarifa kwa umma iliyotolewa na Benki ya Mkombozi ilisema, “Benki ya Mkombozi haijihusishi na haitajihusisha na utakatishaji wa fedha chafu.”
Kuhusu kufunguliwa kwa akaunti hiyo na Rugemalira taarifa hiyo ilisema fedha zote zilizoingizwa kwenye akaunti ya VIP iliyopo kwenye benki hiyo zilitokana na mauziano ya hisa kati ya VIP na PAP kwa mkataba uliotambuliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania.
Ilisema chanzo cha malipo hayo ni kuhamisha fedha kutoka kwenye akaunti ya PAP iliyopo katika benki ya Stanbic na kuingizwa kwenye akaunti ya VIP iliyopo katika Benki ya Mkombozi.
Kuhusu kuhamishwa fedha taarifa hiyo ilisema,“Fedha hizo zilihamishwa katika mafungu mawili, fungu la kwanza ilikuwa ni Sh73.6 bilioni zilihamishwa kwa njia ya TISS kwa kumbukumbu namba 000000050720 ya Januari 23 mwaka huu na fungu la pili ni Dola 22 milioni zilihamishwa kwa TISS kwa kumbukumbu namba 000000050812 siku hiyo hiyo.”
“Malipo mengine ya asilimia kumi ya mauzo ya hisa yalilipwa kwenye akaunti ya Mkombozi iliyopo Benki Kuu ya Tanzania, kutokana na mchakato huo benki ya Mkombozi ilijiridhisha kuwa fedha hizo ni malipo halali na siyo fedha chafu,” ilisema taarifa hiyo.
Iliongeza: “Benki inawataarifu wateja wake na Watanzania kwa ujumla kutoyumbishwa na tuhuma hizo ambazo hazina ukweli ndani yake, badala yake waitumie benki yao kwa shughuli za maendeleo ya nchi yetu.”
- Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم