
Dodoma. Bunge jana lilikabidhi ripoti ya uchunguzi wa IPTL kwa
Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) ili ipitie na kutoa mapendekezo
bungeni, hatua ambayo inatazamiwa kusababisha mtikisiko wa tano katika
Serikali ya Rais Jakaya Kikwete.
Ripoti hiyo iliyoandaliwa na Mdhibiti na Mkaguzi
Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), katika vitabu vitano, ilikabidhiwa na
Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai kwa Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe huku
akimpa masharti ya kuipitia kwa siri, kinyume na Zitto alivyokuwa
ameahidi kuwahoji watuhumiwa katika kikao cha wazi.
Ripoti hiyo inatokana na uchunguzi maalumu wa
fedha zilizochotwa katika akaunti ya escrow ndani ya Benki Kuu ya
Tanzania (BoT), iliyokuwa inatunza fedha za gharama za uwekezaji
(capacity charge) kwa Kampuni ya Kufua Umeme ya IPTL baada ya kutokea
mgogoro wa kibiashara baina yake na Tanesco.
Tanesco ililalamika kuwa ilikuwa inailipa zaidi
IPTL kinyume na gharama za uwekezaji hivyo kuamuliwa na Mahakama kuwa
fedha ilizokuwa inatakiwa kulipa ziwekwe katika escrow hadi upatikane
ufumbuzi wa mgogoro huo.
Hata hivyo, kesi hiyo ilipohukumiwa Februari mwaka
huu, ikibainisha kweli Tanesco ilikuwa inailipa zaidi IPTL, ilibainika
kuwa fedha zilizokuwa katika akaunti hiyo Sh 306 milioni
zilikwishachotwa na IPTL kwa ruksa ya baadhi ya viongozi wa Serikali.
Kutokana na hali hiyo, ripoti hiyo inaweza
kuondoka na vigogo waliohusika na kashfa hiyo, kama ilivyowahi kutokea
katika kashfa nyingine nne zilizoitikisa Serikali ya Awamu ya Nne ya
inayoongozwa na Rais Kikwete
Richmond
Kashfa kubwa iliyotikisa nchi katika kipindi cha
awali cha Rais Kikwete ilikuwa ni Richmond ya mwaka 2006. Hii ilitokana
na tatizo kubwa la uhaba wa umeme na Serikali kulazimika kutafuta njia
za dharura za kutatua tatizo hilo, zikiwamo zilizodaiwa kukiuka taratibu
na sheria.
Baada ya kashfa hiyo kuchunguzwa na taarifa
kutolewa bungeni, aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa alilazimika
kujiuzulu baada ya kutakiwa ajipime kutokana na mazingira ya kashfa
hiyo.
Wengine waliong’oka madarakani ni mawaziri wa Nishati na Madini kwa vipindi tofauti, Nazir Karamagi na Dk Ibrahim Msabaha.
- Soma Zaidi Hapa(Mwananchi)
- Soma Zaidi Hapa(Mwananchi)
إرسال تعليق