Phiri amuondoa Tambwe Simba, mwenyewe agoma

KOCHA wa Simba, Patrick Phiri, aliondoka Dar es Salaam jana Alhamisi usiku kwenda kwao Zambia, lakini akautaka uongozi wake kumwacha huru straika wake Mrundi Amissi Tambwe ili ajiunge na timu nyingine. Hata hivyo mchezaji huyo amegoma.

Phiri aliliambia Mwanaspoti kuwa kwa kipindi alichokaa na Tambwe amemuona ni mchezaji mzuri lakini hana furaha kuichezea timu hiyo tangu kuwepo na taarifa zilizokuwa zikimhusisha kuihujumu timu na ujio wa mshambuliaji Mganda Emmanuel Okwi huku akitajwa yeye kuondoka kwenye usajili uliopita.

Alisema kuwa Tambwe ameathirika kisaikolojia na ameonyesha kutokuwa na furaha ndani ya Simba hivyo ni vyema viongozi wa klabu hiyo wakafanya uamuzi sahihi wa kumruhusu kwenda kuichezea timu nyingine ambayo ataona inamfaa ili kunusuru kiwango chake.

“Niliwahi kuzungumza na Tambwe na aliniambia kuna timu nyingi zinamtaka, hayo yalitokea baada ya kuwepo na maneno mengi juu yake, mpaka sasa Tambwe bado hajakaa sawa kisaikolojia na hana furaha ndani ya timu, mimi kama kocha nafahamu tatizo linaloweza kutokea kwamba anaweza kushindwa kucheza kabisa,” Phiri alisema.

“Ni vyema viongozi wamruhusu kwenda timu nyingine kama atapata kuliko kumlazimisha kuwepo ndani ya Simba, hali hiyo itamshusha kiwango chake kabisa, raha ya kazi ufanye pale ambapo unaona una furaha napo.

“Tambwe bado ni kijana mdogo na uwezo wake ni mkubwa ila kwa sasa kavurugikiwa. Kuendelea kumbakiza Simba ni sawa na kutaka kuua kipaji chake, siwezi kushauri hivyo.”

Lakini kwa upande wake,  Tambwe aliliambia Mwanaspoti akiwa Burundi kwa kusema: “Bado nina mkataba na Simba ambao umebaki muda mfupi kumalizika, sijafanya mazungumzo yoyote na viongozi wangu juu ya kuongeza mkataba mpya, hivyo nitarudi huko Novemba 30 kumalizia mkataba wangu na mengine yatafuata.”

Phiri alipeleka ripoti yake ambayo ilijadiliwa na kupitishwa huku akipendekeza wachezaji kutoka Mtibwa Sugar; Ame Ally na Hussein Kessy, Danny Mrwanda (Polisi Moro) na Mganda Dan Sserunkuma wa Gor Mahia ya Kenya.

Hata hivyo Phiri alitoa baraka kwa viongozi wake kumsaidia kusaka wachezaji watakaoisaidia Simba katika safu ya ushambuliaji, kiungo, beki ya kati na pembeni ambapo alihitaji mchezaji mmoja mmoja kila safu kwa maelezo kwamba sio rahisi kwake kuwafahamu wachezaji wote kwani mechi walizocheza ni chache.

Viongozi wa Simba walianza mchakato wa kusaka wachezaji ambapo tayari wamefanya mazungumzo na Emeh Izuchukwu anayeelezwa kuwa ameomba mwenyewe kurudi Simba, mabeki Salum Kimenya, Nurdin Chona (Prisons), kiungo Deus Kaseke (Mbeya City), Said Morad (Azam) na kipa Juma Kaseja (Yanga).

 Aidha, kuna habari kwamba Sserunkuma anaweza kuziba nafasi ya Tambwe ingawa Mkenya Raphael Kiongera ambaye anatarajia kwenda kufanyiwa upasuaji wa goti na kukaa nje ya uwanja kwa muda mrefu jambo ambalo Phiri amesema linaweza kuigharimu timu.

 Wengine wanaotajwa kutemwa ni Amri Kiemba ambaya anaandaliwa mpango wa  kupelekwa kwa mkopo Azam kama watafikia makubaliano, Nassoro Masoud ‘Chollo’, Uhuru Seleman, Harun Chanongo, Ivo Mapunda, Joram Mgeveke na Pierre Kwizera.
- MwanaSpot

Post a Comment

Previous Post Next Post