Umeme wakatika maeneo mengi nchini

Dar es Salaam. Baadhi ya maeneo nchini yalikosa umeme kwa siku nzima ya jana, kitendo kilichotafsiriwa na wengi kwamba ni hujuma ili kuwafanya wasione mjadala wa kashfa ya IPTL uliokuwa ukiendelea bungeni Dodoma jana.
Taarifa zilizokifikia chumba cha habari, zilieleza kuwa maeneo mengi katika miji ya Mwanza, Arusha, Tanga na baadhi mikoa mingine hayakuwa na huduma hiyo.
Pia, baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam na Morogoro hayakuwa na umeme kwa kutwa nzima ya jana na kusababisha malalamiko mengi ya wananchi.
Chumba cha habari cha Mwananchi, kutwa nzima jana kilikuwa kikipokea simu mbalimbali za wananchi wakitaka kufahamu sababu za kukatika kwa umeme wakati ikifahamika kuwapo kwa mjadala huo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Felchesmi Mramba alithibitisha kukatika umeme katika maeneo mengi ya nchi lakini alikanusha kuwa siyo hujuma kuwafanya wananchi wasipate matangazo ya moja kwa moja kutoka Dodoma.
Alisema kukatika kwa umeme kunatokana na matatizo ya moja kati ya mitambo mitatu ya kuzalisha umeme kwenye Bwawa la Kidatu, Morogoro.
Alisema mtambo huo una matatizo ya kifaa muhimu kiitwacho gavana ambacho kilikuwa kinafanyiwa ukarabati.
“Matatizo ya mtambo huo yako wazi na tulishatangaza kwenye vyombo vya habari kuhusu tatizo hilo na kwamba baadhi ya maeneo yatakosa umeme leo kwa sababu ya matengenezo ya mtambo huo.
“Hata hivi ninavyozungumza, mafundi wako kwenye matengenezo, hata ukitaka kuhakikisha unaweza kutuma mwakilishi wako atawakuta mafundi wakiendelea na matengenezo,” alisema.
Hata hivyo, Mramba hakutaka kuelezea wala hakufafanua maeneo yaliyopaswa kukosa umeme kutokana na matengenezo ya mtambo huo muhimu unaochangia katika gridi ya taifa, akieleza kwamba tayari walishatoa matangazo kwenye vyombo vya habari.
Alisisitiza kupuuza taarifa kwamba kukatika huko kwa umeme ni sehemu ya hujuma ili kuwanyima wananchi fursa ya kufuatilia matukio yanayoendelea bungeni hasa kuhusu mjadala huo IPTL ambao unaigusa Tanesco.
- Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post