Saratani ya tezi dume ni hatari

Dar es Salaam. Pamoja na maelezo ya Rais Jakaya Kikwete aliyotoa juzi juu ya ugonjwa wa saratani ya tezi dume mara baada ya kurejea nchini kutoka Marekani alikotibiwa, maswali kuhusu ugonjwa huo bado ni mengi na hivyo kuhitaji ufafanuzi.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere mara baada ya kuwasili nchini, Rais Kikwete alielezea hali yake, jinsi alivyogundulika kuwa na saratani ya tezi dume na matibabu aliyoyapata.

Rais Kikwete anastahili pongezi kwa namna alivyovunja ukimya na amesaidia kujua umuhimu wa kujali afya zetu na kuweka wazi hali zetu za kiafya, si kwa tezi dume pekee, bali pia maradhi mengine.

Maana ya saratani

Saratani maana yake ni ukuaji holela bila mpangilio wa seli baada ya kuparanganyika kwa mfumo wa seli unaodhibiti ukuaji na uhai wake. Na uvimbe wa kawaida wa tezi maana yake ni kuwa seli zimetutumka tu lakini hakuna mparanganyiko wa seli wala kukua kwa kusambaa kiholela kama ilivyo kwa saratani.

Hivyo, ndio maana kuna tatizo la kuvimba tezi dume na wengine kupata saratani ya tezi dume kwa wanaume wenye umri mkubwa.

Tezi dume ni sehemu mojawapo ya mfumo wa uzazi wa kiume. Inaundwa na sehemu mbili ambazo zimeunganishwa na kufunikwa kwa nje kwa utando wa tishu.

Tezi hii ipo mbele kidogo ya puru (rectum) na chini kidogo ya kibofu cha mkojo. Tezi dume inauzunguka mrija unaounganisha kibofu cha mkojo na uume (urethra).

Kazi ya tezi dume

Mojawapo ya kazi za tezi dume ni kutoa majimaji yanayochanganyika na mbegu za kiume (sperms) wakati wa kilele cha tendo la kujamiana. Mchanganyiko huu wa mbegu pamoja na majimaji hayo hutengeneza shahawa (semen).

Majimaji hayo husaidia kuzipa mbegu za kiume nguvu ya kusafiri kwenye uke mpaka kufikia kwenye mirija ya uzazi, tayari kwa utungisho na yai la kike. Vilevile husaidia kupunguza hali ya kitindikali iliyopo katika uke, ambayo isiporekebishwa, huua mbegu nyingi za kiume na kufanya utungisho kuwa wa tabu.

Saratani ya tezi dume inashika nafasi ya tatu kwa kusababisha vifo vinavyotokana na saratani kwa wanaume wa umri mbalimbali duniani.
- Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم