Dar es Salaam. Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi),
imeiagiza mikoa yote nchini kuwasilisha taarifa kuhusu kasoro
zilizojitokea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa juzi ili iwachukulie
hatua watendaji watakaobainika kuhusika.
Imesema kushindwa kusimamia uchaguzi na
kusababisha kasoro, ni moja ya makosa makubwa na kuwa watakaobainika,
watachukuliwa hatua kali kulingana na uzito na kiwango cha kuhusika kwao
na kwamba wanaweza kufukuzwa kazi, kuvuliwa madaraka, kushushwa cheo au
kukatwa mishahara.
Uchaguzi huo ulikumbwa na kasoro nyingi na
kuahirishwa katika baadhi ya maeneo kutokana ama kukosekana kwa majina
ya wagombea, baadhi yao kuwekewa nembo za vyama wasivyotoka au uhaba wa
vifaa vya kupigia kura.
Hata hivyo, halmashauri 145 kati ya 162
zilizofanya uchaguzi huo hazikuwa na dosari, tatu hazikufanya uchaguzi
kabisa kutokana na vifaa kuchelewa, 14 zilikuwa na kasoro katika baadhi
ya vijiji, vitongoji na mitaa na uchaguzi wake kuahirishwa mpaka Desemba
20 na 21. Akitoa taarifa ya awali ya uchaguzi huo, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia alisema pamoja na kasoro
hizo, uchaguzi huo umefanikiwa kwa zaidi ya asilimia 80.
“Katika uchaguzi huu hakukuwa na vitambulisho vya
mpigakura kama ilivyo katika Uchaguzi Mkuu. Uchaguzi huu unafanyika
katika mtaa au kitongoji hivyo ni rahisi watu kutambuana na pia mtu
akishapiga kura si rahisi kurudia mara ya pili na tuliagiza mpigakura
awe ama na kitambulisho cha kazi, leseni au kile cha kupigia kura katika
Uchaguzi Mkuu kwa ajili ya kutambulika,” alisema.
Alisema malalamiko na kasoro zilizoripotiwa katika
vyombo vya habari haziwezi kujibiwa wala kutolewa ufafanuzi na Tamisemi
hadi baada ya kupata ripoti kutoka mikoani.
Akizungumzia malalamiko ya wananchi kutoyaona
majina yao, Ghasia alisema ulitolewa muda wa siku tatu kwa wananchi
kufanya uhakiki lakini wengine hawakufanya hivyo.
“Kuhusu majina kubadilishwa au kuisha kwa wino na
kukosekana kwa vitu vidogovidogo hilo linaweza kuwa limefanyika kutokana
na uzembe tu. Ndiyo maana tumeagiza tupewe taarifa rasmi.”
Akizungumzia kasoro zilizobainika katika karatasi
za kupigia kura, alisema utaratibu wa kuandaa vifaa hivyo ulikuwa
ukifanywa na halmashauri husika na si Tamisemi, hivyo ni vigumu kwa
wizara hiyo kuagiza walioandaa vifaa wachukuliwe hatua.
“Mfano Temeke na Ilala walimtumia Mpigachapa Mkuu
wa Serikali. Awali, aliwapelekea vifaa vyenye matatizo, hata
walipovirejesha ili avirekebishe, vilirudishwa vikiwa bado na kasoro.
Mpiga Chapa aliingia mkataba na manispaa na ndiyo aliyepewa zabuni,”
alisema.
Alisema suala hilo linafanyiwa uchunguzi ili
kubaini kama kasoro katika wilaya hizo zimesababishwa na Mpiga Chapa wa
Serikali au wilaya husika.
Alipotafutwa mpiga chapa mkuu wa serikali, Cassian
Chibogoyo kuzungumzia kuhusu tuhuma za ofisi yake kuwa sehemu ya dosari
za uchaguzi katika manispaa za Ilala na Temeke, alisema tuhuma
amezisikia na kwamba atawasiliana na wizara kabla ya kutoa majibu yake
leo.
- Mwananchi
- Mwananchi
إرسال تعليق