Kitabu cha ‘urais’ wa Makamba

Dar es Salaam. Ni dhahiri mpambano wa kuwania urais ndani ya CCM unazidi kunoga, ikiwa imebakia miezi michache kabla ya kupulizwa rasmi kipenga.
Mmoja wa makada kutoka CCM waliotangaza nia ya kuwania kiti hicho, January Makamba ameandikiwa kitabu kinachoeleza nia yake hiyo.
Kitabu hicho pamoja na mambo mengine kinaeleza mikakati ya mwanasiasa huyo kijana iwapo atapitishwa na chama chake ili kuwania na hatimaye kushika nafasi hiyo ya juu ya uongozi kitaifa.
Katika kitabu hicho chenye kurasa 196, Makamba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Mbunge wa Bumbuli, Tanga anasema rais ajaye lazima awe na tafakuri pana na nia ya kuendeleza nchi na siyo kuwa na kaulimbiu nyepesi za afya bure, elimu bure zisizo na ufafanuzi ili kuwahadaa wananchi.
Kitabu hicho kilichoandikwa na mchambuzi na mwandishi wa makala za siasa, Padri Privatus Karugendo kimebeba sera na mikakati yake kiundani ya kuiongoza nchi iwapo atapatiwa dhamana na CCM kugombea urais.
Katika kitabu hicho kinachoitwa, ‘Maswali na Majibu 40: Mazungumzo na January Makamba kuhusu Tanzania Mpya’, mwanasiasa huyo anasema uongozi hauishii kwa kauli za juu juu za kuongeza ajira, kuboresha elimu kwani kila mtu anaweza kuyasema hayo.
Anamwonaje rais ajaye
Anasema katika tafakuri zake anaona rais ajaye anatakiwa kuzitambua kwa kina changamoto za nchi yake na kuwa na mikakati ya kuzitatua.
Changamoto hizo, Makamba anasema ni za kiuongozi na utatuzi wake unategemea kiongozi mwenyewe, hulka, mtazamo wake na usahihi wa uamuzi anaoufanya.
“Kuomba uongozi wa nchi siyo harakati binafsi na wafuasi wako kupata vyeo. Ni dhamana kubwa ya kujenga mustakabali wa nchi na kuwaunganisha Watanzania wote. Kwa hiyo, uamuzi wa kugombea lazima uupe heshima na nafasi inayolingana na dhamana yenyewe,” anasema Makamba kwenye kitabu hicho.
Anaongeza kuwa rais anatakiwa kuongeza kasi ya kuondoa umaskini, kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali, vyombo vya dola na mahakama na hayo yatadhihirika kwa vitendo vya kuchukua hatua dhidi ya viongozi wabadhirifu, walarushwa na kudhibiti matumizi ya Serikali.
- Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم