Tutabaki Washangiliaji Afcon hadi lini ?

Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika inayoendelea nchini Guinea ya Ikweta inazidi kupamba moto. Kama kawaida yetu, Tanzania tumeendelea kuwa watazamaji.
Mara ya mwisho Tanzania ilikuwa kwenye michuano hiyo mwaka 1980, ilipofanyika nchini Nigeria. Tangu wakati huo, hatujawahi tena kushiriki fainali hizo.Kwa mashabiki wa soka wanaofuatilia fainali hizo, watakubali kuwa safari yetu ya kucheza fainali hizo kwa mara nyingine ni ndefu na inayohitaji maandalizi ya muda mrefu.
Kwa namna soka letu lilivyotawaliwa na mambo mengi ya nje kuliko uwanjani, ni rahisi kushawishika kuamini kuwa tuna safari ndefu kabla ya kufikia mafanikio.
Mafanikio ya mchezo wa soka siyo sawa na bahati ya mtu kulala maskini na kuamka tajiri. Hakuna njia ya mkato kufanikiwa katika soka kama wengi wanavyoweza kufikiria.
Tunaendelea kuwa watumwa wa kushindwa kukubali ukweli kwamba, safari yetu ya kurejea mbio za mwaka 1980, hazihitaji longolongo na porojo za kujifurahisha kutoka kwa viongozi wetu.
Ushindani unaoonekana kwenye mashindano hayo, unatufanya tuamini kuwa bila juhudi na kujituma, tunaendelea kuwa mashuhuda wa fainali hizi kupitia televisheni kila siku.
Leo hii viongozi wetu wamebaki kupiga kelele za ukata kila kukicha. Inasikitisha kiongozi anakosa ubunifu wa kutafuta njia za kuhakikisha michezo inasonga mbele, badala yake analia njaa.Viongozi wanasahau kuwa wana dhamana yao ya kuongoza ni pamoja na kuwa wabunifu katika kuhakikisha mafanikio yanapatikana. Kwa viongozi wetu hilo hawana.
Katika hali kama hiyo unategemea lini Taifa litasonga mbele? Viongozi wamebweteka ofisini, hawaendi viwanjani na kujifunza mambo yanayotokea huko.
Soka letu limejaa fitina nyingi, kuanzia ndani ya uwanja hadi nje. Kila kitu tunakichukulia kwa uzito mwepesi, maswali magumu tunayaandalia majibu mepesi, halafu tunataka kwenda Fainali za Kombe Mataifa ya Afrika.
Hivi tunadhani ni lini tutakwenda kufanikiwa kama wale ambao walipaswa kuwa mfano mzuri wanafanya mambo kinyume chake? Leo hii mwamuzi wa soka kuchezesha mechi analazimika kujishauri zaidi ya mara mbili kwa hofu ya kupigwa na wachezaji kwa madai ya upendeleo.
Hatuna sababu ya kupata shida kuamini kuwa, wachezaji wanaofanya hivyo wanaandaa Taifa la vijana wa fujo viwanjani. Tunawajengaa nidhamu mbaya, kwamba kama mwamuzi amekosea basi adhabu yake ni kupigwa.
Ni badiliko tu ndiyo yatakayokomboa soka la Tanzania

Post a Comment

أحدث أقدم