Vita ya urais yashika kasi mtandaoni, Wanaotajwa wafungua akaunti za kuwanadi


Dar es Salaam. Wakati safari ya kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu ikipamba moto, kumeibuka makundi ya watu yaliyofungia akaunti katika mitandao ya kijamii yakiwaunga mkono baadhi ya wanasiasa waliotangaza au wanaotajwa kuwa na nia ya kugombea urais ya kuwashambulia washindani wao.
Kila kundi limejipatia wafuasi wengi ambao wanaonyesha kumkubali mwanasiasa husika wanayedhani anafaa kuwa rais wa Tanzania endapo atapitishwa na chama chake na kupigiwa kura na wananchi.
Hata hivyo, wasomi na wachambuzi wanaonya kuwa pamoja na njia hii kuwa ya haraka kuwafikia wapigakura walio wengi ambao ni vijana na wanawake, inatakiwa kutumika kwa uangalifu la sivyo inaweza kusababisha machafuko.
Makundi yenyewe
Makundi hayo, mengi yakipatikana katika mitandao ya Facebook, Twitter na WhatsApp yanafanya kazi ya kuwanadi wanasiasa na kubainisha shughuli mbalimbali wanazozifanya kila siku wawapo katika ziara zao za binafsi, za kiserikali au kichama katika maeneo mbalimbali nchini.
Baadhi ya kurasa za makundi hayo zenye wafuasi wengi ni pamoja na ule wa ‘Team Lowassa’, kundi linalomuunga mkono Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa ambao hadi jana ulikuwa na wafuasi 46,124 ambao wanaweza kupata habari mbalimbali zinazomhusu kiongozi huyo.
Hata hivyo, mbunge huyo ambaye pia aliwahi kuwa waziri mkuu, hivi karibuni alikaririwa na gazeti hili akiikana moja ya akaunti za Twitter iliyokuwa imechapisha taarifa zilizomkariri akizungumzia suala la ufisadi wa escrow.
Akizungumzia kurasa hizo, Msaidizi wa Lowassa, Abubakar Liongo alisema akaunti hizo zinatengenezwa na marafiki na kusisitiza kwamba kiongozi huyo hahusiki nazo kwa namna yoyote.
“Hawa ni marafiki tu, huwezi kuwazuia kufanya wanachotaka kufanya, sisi tumeshatoa taarifa kuwa hizi hatuhusiki nazo,” alisema Liongo.
Kundi jingine linajitambulisha kama ‘Team Hamis Kigwangalla’ linalomuunga mkono Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla na mpaka kufikia jana lilikuwa na wafuasi 9,893. Hili ni kundi la pili kuwa na wafuasi wengi katika mtandao wa Facebook baada ya lile la Team Lowassa.
Ukurasa mwingine umeanzishwa na watu wanaomuunga mkono Mbunge wa Bumbuli na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba. Ukurasa huu umepewa jina ‘January Makamba – The next President’ na hadi jana ulikuwa na wafuasi 7,075.
Wanasiasa wengine wanaohusishwa na mitandao hiyo ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ambaye mbali na akaunti yake kwenye WhatsApp, ukurasa wa marafiki zake kwenye Facebook wenye jina la ‘Bernard Membe Fans Page’ umefikisha wafuasi 5,120.
- Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم