Mkazi wa Kitongoji cha Nyamorege kilichopo Mtaa wa
Forodhani mji mdogo wa Sirari Wilaya ya Tarime mkoani Mara, Marwa
Kihiri Mwita, anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumuua baba yake
mzazi Kihiri Mwita kinyama kwa kumpiga na koleo kichwani na ubavuni.
Vilevile inadaiwa kuwa mtuhumiwa huyo alijeruhiwa kwa kucharangwa
kwa panga na baba yake huyo kabla ya kumjeruhi kwa kumpiga na koleo
kichwani na ubavuni baada ya kuzuka ugomvi baina yao.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Forodhani Sirari, Nyangoko Paulo
alithibitisha kutokea kwa tukio hilo Ijumaa ya wiki iliyopita jioni
katika kitongoji hicho.
Paulo alisema kuwa ugomvi huo uliibuka baada ya baba kumtuhumu mwanaye kuwa anatabia ya wizi.
Alisema inadaiwa kuwa baba huyo alimweleza mwanaye huyo kuwa
aliwahi kufanya wizi kitendo kilichosababisha kutozwa faini ya ng'ombe.
Paulo alisema inadaiwa kuwa baada ya baba kutoa tuhuma hizo, mwanaye alitoroka na kuwa nje ya familia kwa zaidi ya miaka mitano.
Alisema aliporudi nyumbani kwao, baba alikerwa na kuanza kumfukuza
kwa panga ili asiingie ndani kwake huku akisisitiza aende akaishi kwa
wahalifu wenzake.
Mwenyekiti alisema baba akirusha panga na kumkata mkononi, mwanawe alichukua koleo na kumpiga nalo kichwani na ubavuni.
Alisema majirani walijitokeza kumuokoa na kuwakimbiza Hospitali ya
Wilaya Tarime ambako alikufa kabla ya kuanza kupatiwa matibabu.
Polisi Tarime Rorya wamethibitisha kutokea kwa mauaji hayo na
kumshikilia mtuhumiwa huyo kwa mahojiano kisha atafikishwa mahakamani
kujibu mashtaka.
AUAWA DUKANI
Nao; Hassan Maulid (32), Hamad Hussein (25), Rashid Yusuph (21) na
Abdallah Swalehe (25), wakazi wa Kijiji cha Porobanguma Wilaya ya Chemba
mkoani Dodoma, wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumuua
mfanyabiashara, Asheli Magina (40) kisha kumpora pikipiki na bidhaa
mbalimbali baada ya kumvamia dukani alikokuwa amelala.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime, alisema kuwa
mtuhumiwa Maulid maarufu kwa jina la Salama, alikuwa akitafutwa na
jeshi hilo kwa kuhusishwa na mauaji ya Ijumaa Said (30), mkazi wa
kijiji cha Monjore – Banguma kwa kumchoma kwa kisu.
Kwa mujibu wa Kamanda huyo, Said aliuawa Januari 19, mwaka huu
majira ya saa 12:30 jioni katika kijiji cha Porobanguma baada ya
kuibuka ugomvi kati yao.
Akizungumzia kuhusu mauaji ya Magina ambaye alikuwa mfanyabiashara
na mkulima wa kijiji cha Bubutole, alisema yalitokea Februari 11, mwaka
huu usiku kwa kucharangwa mapanga kichwani na mikononi baada ya
kumvamia nyumbani kwake wakati amelala dukani.
Alisema baada ya mauaji hayo, watuhumiwa hao wanadaiwa kupora
pikipiki na bidhaa mbalimbali dukani hapo ambavyo thamani yake
haijajulikana.
Misime alisema watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa na pikipiki hiyo T. 449 CQP aina ya SUNLG na bidhaa hizo mali ya marehemu huyo.
Alisema watuhumiwa hao pia walionyesha panga linalodaiwa kutumika katika mauaji ya Magina.
Alisema watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani baada ya upelelezi wa mauaji hayo kukamilika
إرسال تعليق