Nilimrekodi Ponda kwa tahadhari - Shahidi

Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Ponda Issa Ponda.
Shahidi wa nane katika kesi ya jinai inayomkabili Katibu  wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Ponda Issa Ponda (pichani),  ameieleza Mahakama ya Hakimu mkazi mkoa wa Morogoro namna alivyofanikiwa kurekodi mkanda wa video kwa siri kwa kutumia kamera ndogo ambayo ilikuwa siyo rahisi kuonekana kwa watu.
Ameeleza mahakamani kuwa wakati akichukua mkanda huo wa video alichukua taadhari kubwa huku akiwa amevalia nguo za kiraia  baada ya kutadharishwa na mkuu wake wa kazi kuwa tukio hilo linaweza kuhatarisha maisha yake, hivyo ni muhimu kuwa na tahadhari kubwa wakati wa kurekodi mkanda huo.
 Shahidi huyo ambaye ni Askari polisi G1293 D/C Abdalah, anayefanyakazi Ofisi ya Upelelezi mkoa wa Morogoro, alieleza mbele ya Hakimu wa Mahakama hiyo, Mary Moyo, kuwa ilikuwa ni lazima kurekodi Kongamano la Eid pili ambalo Sheikh Ponda alitoa maneno  yenye kuumiza imani za dini nyingine na pia alishawishi watu kutenda kosa.
Akiongozwa na Wakili Mkuu Mwandamizi wa Serikali, Benard Kongola, alidai kuwa Agosti 10, 2013,  jioni alipewa maelekezo na mkuu wake wa kazi na kutakiwa kwenda kurekodi video kwenye kongamano hilo hivyo alichukua kamera ndogo aina ya JVC ambayo haikuwa rahisi kuonekana kwa watu.
Alisema alifika eneo la tukio na kuungana na waumini wengine kama mmoja wa wasikilizaji wa kongamano hilo na kuanza kutoa kamera hiyo kwa siri kisha kurekodi tukio hilo mpaka lilipomalizika bila kutambuliwa na mtu yoyote katika eneo hilo.
Alidai kuwa kama alivyoelekezwa na mkuu wake wa kazi, baada ya kumaliza kurekodi  kongamano hilo alirudi ofisini akiwa na  kamera hiyo na kumkabidhi mkuu wake wa kazi.
 Wakili wa Utetezi, Abubakari Salimu alimuuliza Shahidi huyo, kama alitumwa kurekodi video katika kongamano hilo je, hakusikia mlio wa bomu, na je, kamera na shahidi kipi kinaweza kutunza kumbukumbu.
 Akijibu maswali hayo shahidi huyo alieleza kuwa kazi yake ilikuwa ni kwenda kurekodi na siyo kusikiliza milio ya mabomu na kwamba yeye siyo mtaalamu wa mabomu, hivyo hawezi kutofautisha mlio wa bomu na gurudumu la gari likipasuka. 
Kesi hiyo itaendelea Februari 26, mwaka huu

Post a Comment

أحدث أقدم