Jeshi la Polisi lijisafishe

GAZETI hili jana tulichapisha ripoti ya utafiti iliyokuwa ikieleza kuwa Jeshi la Polisi nchini limeingia lawamani kutokana na kudaiwa kuwa linahudumia zaidi watu wenye fedha kuliko wananchi wa kawaida.
Utafiti huo uliofanywa na Taasisi ya Twaweza unaonyesha kuwa wananchi sita kati ya 10 sawa na asilimia 60 wanaamini jeshi hilo linawahudumia zaidi watu wenye fedha kuliko Watanzania wa kipato cha chini.
Pia, kwa mujibu wa utafiti huo matukio ya ukatili dhidi ya polisi yameongezeka, wananchi wawili kati ya 10 ambao ni asilimia 21 wamesikia matukio ya aina hiyo na kwamba mwaka jana ni mwananchi mmoja kati ya 10 aliyeyasikia matukio kama hayo.
Utafiti huo unaonyesha kuwa kutokana kupungua kwa imani na jeshi la polisi, watu wengi wameamua kuanzisha vikundi vya usalama vya kijamii ambavyo husimamia utekelezaji wa sheria za kawaida ambako wanaripoti matuko hayo.
Tunachukua nafasi hii kuipongeza Taasisi ya Utafiti ya Twaweza kwa kufanya utafiti huu ambao umetoa picha ya hali ilivyo ndani ya jeshi la polisi nchini.
Hii sio mara ya kwanza kwa tafiti mbalimbali zilizowahi kufanywa kuinyoshea kidole jeshi la polisi kwamba linahusika na ukiukwaji wa haki za binadamu au linajihusisha na vitendo vya rushwa.
Mwanzo nwa mwaka huu Taasisi ya Afrobarometer ilitoa ripoti ya utafiti wake ukionyesha kuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ni kati ya taasisi zilizoshika nafasi za juu kwa kupokea rushwa katika kipindi cha miaka 10 iliyopita. Utafiti huo ulilihusisha jeshi la polisi katika vitendo hivyo.
Tunachukua nafasi hii kulitaka jeshi la polisi kutumia ripoti za tafiti hizi kujitathmini na kuchukua hatua za kujisafisha.
Tunaamini kuwa tafiti hizi zote zimefanywa kisayansi kwa kuwauliza wananchi ambao majibu ndiyo yamekuwa msingi wa ripoti hizi.
Jeshi la polisi kazi yake ni kulinda raia na mali zao, lakini linapoanza kuhusishwa na vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu na kupokea rushwa, ni hatari sana katika ustawi wa nchi.
Ni wazi kuwa wananachi watapoteza imani na jeshi hilo na matokeo yake wananchi wanaweza kujiingiza katika vitendo vya kujichukulia sheria mkononi.
Hivi sasa wananchi wanapomkamata mhalifu humkumu kwa kumchoma moto au kumuua kwa kipigo wakiamini kuwa wakimpeleka polisi huenda akaachiwa.
Ni vyema sasa jeshi la Polisi lijisafishe kwa kuwaondoa kazini askari ambao wanajihusisha na rushwa na vitendo vingine ambavyo vinalipaka matope, ili wananchi waendelea kuliamini na kutoa ushirikiano wa kudhibiti wahalifu.
- Jamboleo

Post a Comment

Previous Post Next Post