Serikali yasalimu amri, yasitisha nauli mpya.

Mkurugenzi Mkuu, Gilliard Ngewe.
Siku tatu baada ya Chama cha Wamiliki wa Mabasi yaendayo mikoani (Taboa), kuendelea na msimamo wa kugoma nchi nzima kupinga nauli mpya, Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), imenywea na kufuta agizo lake la awali la kupunguza nauli hizo.
 
Badala yake, Sumatra imetangaza kusitishwa utekelezaji wa viwango vipya vya nauli vilivyotangazwa hivi karibuni na kutaka vya zamani viendelee.
 
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Sumatra kwa vyombo vya habari, jana jijini Dar es Salaam, na kusainiwa na Mkurugenzi Mkuu, Gilliard Ngewe, utekelezaji utasitishwa hadi marejeo yatakapofanyika tena.
 
“Sumatra imepokea kutoka kwa msafirishaji ABC Trans na Afritrans Limited maombi ya kupitia upya maamuzi yake ya kushusha viwango vya nauli za mabasi ya masafa marefu yalitolewa kwa Agizo Na. SMTRA/02/2015 la Aprili 15, mwaka huu.  Maombi ya Kampuni mbili yalipokelewa Sumatra Aprili 29, mwaka huu, kwa mujibu wa Kifungu Na 19 (2)(b) cha Kanuni za Tozo za mwaka 2009,” alisema.
 
Alisema kwa sasa viwango vya nauli vya zamani vitaendelea kutumika hadi hapo umma utakapotaarifiwa vinginevyo.
 
Afisa Uhusiano wa Sumatra, David Mziray, alisema sheria inatoa haki kwa wahusika kukata rufaa ndani ya siku 14 na kwamba kwa sasa wanapitia hoja zao kuona kama zina mashiko ndipo watatoa maamuzi ambayo yatawekwa wazi.
 
Alisema viwango vipya vya nauli vilitolewa baada ya kukokotoa na kwamba kwa mujibu wa kanuni na kwamba mambo yatawekwa wazi ndani ya siku 14.
 
Aprili 15, mwaka huu, Sumatra ilitangaza viwango vipya vya nauli ambavyo vilipaswa kuanza kutekelezwa jana, kwa kupandisha nauli za mabasi huku za usafiri wa mijini ukibaki kama ulivyo.
 
Aprili 27, mwaka huu, Taboa ilitangaza mgomo nchi nzima kupinga maamuzi ya Sumatra ya nauli mpya.

Post a Comment

أحدث أقدم