Sumaye: Upinzani wataingia Ikulu CCM Wakipitisha mtoa Rushwa


WAZIRI Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye amekionya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutopitisha mgombea  urais   kwa njia ya rushwa kwa vile  kufanya hiyo kutawaingiza wapinzani Ikulu.

Sumaye ambaye ni miongoni wa makada wanaowania   kuteuliwa  na CCM kugombea nafasi  hiyo,  aliyasema hayo juzi  mjini Bariadi  alipowashukuru  wana CCM  45 waliomdhamini mkoani hapa .

Akizungumza  na baadhi ya viongozi wa chama hicho  na wadhamini hao, aliwashukuru waliomdhamini na kueleza kuwa ikiwa CCM itapitisha wagombea kwa njia za rushwa utakuwa mwanzo wa vyama vya upinzani kuchukua nchi.

“Nyinyi  kama wajumbe wa NEC  mtambue kuwa Tanzania kwa sasa tunahitaji kiongozi atakayetuvusha,  tukichagua kwa rushwa tunawapatia wapinzani nafasi kuingia Ikulu  hivyo chama changu kinapaswa kisipitishe mtu kwa rushwa,”alisema.

Alisema sababu kubwa itakayofanya wapinzani kuongoza nchi ni rushwa ndani ya CCM aliyoeleza kuwa imekithiri kwa kiwango kikubwa hasa kwa sasa kuelekea  kipindi cha Uchaguzi Mkuu.

“Sijatoa rushwa tangu nianze kutafuta wadhamini , watu wanajitolea tu kwa mapenzi yao kunidhamini sina haja ya kuwanunua watu ninaowapata nawashukuru kwa maana mapenzi yametoka kwao kunidhamini siyo kwa sababu fulani, ”alisema

Post a Comment

Previous Post Next Post