Rais Magufuli Kukutana na Wafanyabiashara Leo

 


RAIS John Magufuli anatarajiwa kukutana na wafanyabiashara na wawekezaji jijini Dar es Salaam leo. Hii itakuwa mara ya kwanza kwa Rais kukutana na ujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji tangu aingie madarakani.

Taarifa iliyotolewa jana na Baraza la Biashara la Taifa (TNBC) jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli atakutana na jumuiya hiyo Ikulu kwa nia ya kufahamiana na kuona namna ya kushirikiana kufikia malengo ya maendeleo katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Katibu Mtendaji wa TNBC, Raymond Mbilinyi alisema katika taarifa hiyo kuwa, Rais Magufuli anataka kuzungumza na jumuiya hiyo, kujadiliana kwa pamoja ili kuwa na picha ya namna ya kufikia maendeleo yanayotarajiwa.

“Serikali kama mdau mkubwa sana wa masuala yanayohusu biashara na uwekezaji, inataka kufahamu kero zilizopo ili kuongeza kasi ya kuzitatua,” alisema Mbilinyi katika taarifa hiyo.

Akifafanua zaidi alisema, serikali ya awamu ya tano inaamini katika ushirikiano wa dhati wa sekta binafsi na umma kutaleta ustawi wa nchi na watu wake. Katika hotuba ya ufunguzi wa Bunge la 11, Rais Magufuli alielezea nia ya serikali yake kufanya kazi kwa karibu na wafanyabiashara na wawekezaji nchini.

TNBC ambayo Rais ndiye Mwenyekiti wake, ni chombo kilichoundwa kwa shabaha ya kujenga jukwaa la majadiliano kati ya sekta binafsi na umma.

Post a Comment

Previous Post Next Post