Pichani
ni Mohammed Dewji alipokuwa mgeni rasmi wa tamasha la Simba Day,
akisalimiana na mmoja wa wadau kwenye jukwaa kuu. Kulia ni Nyange
Kaburu. (Picha na Maktaba yetu).
Na Rabi Hume, Modewjiblog
Mmoja
wa mashabiki wa wakongwe wa klabu ya Simba, Stanbul Mponda amemuomba
Bilionea namba moja nchini, Mohammed Dewji ‘MO’ kuendeleza mipango yake
ya kuinunua Simba ili aweze kufanya uwekezaji kama alivyokuwa amepanga
awali.
Mponda
ameyasema hayo ikiwa ni siku chache zimepita za tarehe ya mwisho ambayo
aliiota MO kwa uongozi wa Simba kutoa majibu kama wanamuuzia hisa za
klabu hiyo na kama watakuwa hawajatoa majibu atafutilia mbali mpango
wake wa kuinunua Simba.
Akizungumza
na kipindi cha michezo cha E Sports kinachorushwa na redio ya E Fm,
Mponda alisema wanafahamu kuwa MO amekuwa mtu ambaye ana mapenzi ya
dhati na Simba na hivyo kucheleweshwa kutolewa kwa majibu na uongozi wa
Simba isiwe sababu ya yeye kuacha kuinunua klabu hiyo kongwe nchini.
“Dewji
ni mwanachama wa muda mrefu wa Simba tunaelewa ni jinsi gani anaipenda
Simba, asilimia zaidi ya 85 ya sisi wanachama wa Simba tunakubaliana na
wazo la MO na tunajua ana nia ya kuisaidia Simba na hata soka la sasa
limebadilika tofauti na zamani hivyo ni sahihi anavyotaka kufanya na
mimi nitumie fulsa hii kumuomba MO abadilishe mawazo yake na aendelee
kuwa na nia ya kuinunua Simba na sisi tupo nyuma yake,” alisema Mponda.
Aliongeza
kuwa MO amekuwa mwanachama wa muda mrefu wa Simba na anatambua taratibu
za Simba hivyo anapaswa kuwa na subira ili kabla ya klabu kufikia
uamuzi wa kukubali kuiuza klabu, mashabiki wa Simba ambao katika katiba
ya klabu hiyo ndiyo wanajulikana kama wamiliki wa klabu wanatakiwa
kuzungumza kwa pamoja na kutoka na jibu moja juu ya kukubali au kukataa
kuiuza timu yao.
Post a Comment