Wasomi, wanaharakati waeleza dosari zilivyoathiri uchaguzi

Baadhi ya wasomi na wanaharakati wamesikitishwa na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ulivyokuwa na dosari zinazofanana katika maeneo mengi ya nchi na kueleza wasiwasi wao kuwa huenda kulikuwa na njama za kuvuruga uchaguzi huo.
wasomi
Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Ruaha (RUCU) Iringa, Profesa Gaundence Mpangala anasema uchaguzi huo umekuwa mbaya katika maeneo mengi, lakini jambo la kushangaza dosari zilizosababisha hali hiyo zinafanana.
“Inaonekana kwamba kulikuwa na mtandao maalumu uliokuwa umepangwa kuvuruga uchaguzi huo kwa namna hiyo, haieleweki ukiambiwa kwamba vifaa vinachelewa kufika katika vituo vya Dar es Salaam,” anasema Mpangala na kuongeza:
“Bila shaka huo ulikuwa ni mkakati wa kuvuruga, hasa baada ya kuonekana kwamba uchaguzi wa safari hii una ushindani mkubwa ikilinganishwa na chaguzi za Serikali za mitaa zilizopita.”
Anasema kwa hali iliyojitokeza inathibitisha kuwa Tume huru ya Uchaguzi inahitajika kwa ajili ya uchaguzi ujayo, hata kama Katiba Mpya haitapitishwa.
Dk Banna
Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Dk Benson Banna anasema matokeo ya uchaguzi huu yanafungua ukurasa mpya, unaonyesha dalili za wananchi kukichoka Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Ingawa inaelezwa kwamba CCM inaongoza, lakini vyama vya upinzani navyo vimejitahidi kuonyesha nguvu kwa kunyakua mitaa iliyokuwa inashikiliwa na chama tawala, vyama vinavyounda Ukawa vimezidi kupanda hasa Chadema imechukua idadi kubwa,” anasema Banna.
Anasema matokeo hayo ni changamoto kubwa kwa CCM, katika uchaguzi mkuu ujao mabadiliko makubwa yatashuhudiwa, hivyo hali ya mashaka itakikumba zaidi chama hicho kama kisipojipanga vizuri.
“Pia nafikiri kwa kasoro zilizojitokeza kuna haja ya Serikali kuona kwamba umefika wakati uchaguzi huo ukasimamiwa na Tume ya Uchaguzi badala ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,” anasema.
Dk Banna anawashawishi wananchi kuwa na hali ya uvumilivu kwa kufuata sheria mahali ambapo wanabaini matatizo badala ya kushiriki vurugu na kusema ni busara kufanya siasa za kistaarabu.

Post a Comment

أحدث أقدم