MAKAMU wa Rais
, Dk. Mohammed Gharib Bilal amesema haoni sababu
yoyote kwa watu wanaohubiri kuwa hawataki Muungano kukimbilia kuchoma
makanisa na kuvunja baa.
, Dk. Mohammed Gharib Bilal amesema haoni sababu
yoyote kwa watu wanaohubiri kuwa hawataki Muungano kukimbilia kuchoma
makanisa na kuvunja baa.
Hayo aliyasema jana jijini Dar es Salaam wakati alipotakiwa kutoa
maoni yake juu ya vurugu za Zanzibar na waandishi wa habari, alipokutana
na kufanya mazungumzo na ujumbe wa watu saba kutoka Marekani
ulioongozwa na Seneta kutoka Delaware, Christopher Coons.
Alisema kuwa, kikundi cha watu hao kimekuwepo siku nyingi na kinatumia kivuli cha dini katika kufanya siasa.
Makamu wa Rais alieleza kuwa, Zanzibar ni kisiwa kidogo na kupitia
Muungano wananchi wananufaika na kamwe serikali ya awamu ya nne haiwezi
kuvumilia kuona watu wachache wenye agenda iliyojificha wakiharibu jambo
bora lililofanyiwa kazi kwa zaidi ya miaka 48.
“Kila ukipita mikoani unakutana na Wazanzibar wanaishi, kupitia
Muungano tumefungua fursa nyingi. Sioni sababu ya watu kuibuka sasa
kuupinga, na tena kwa kufanya fujo. Tutaendelea kudhibiti hali hii na
kuhakikisha kuwa amani inabakia katika nchi yetu,” alisema Dk. Bilal.
Katika mazungumzo yake na ujumbe huo wa Marekani, Dk. Bilali alielezea
kufurahishwa kwake na uhusiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na
Marekani na pia akafafanua kuwa taifa hilo limekuwa ni rafiki wa kweli
kwa Tanzania kutokana na michango yake ya maendeleo iliyopo nchini.
Alisema Serikali ya Tanzania inaona faraja kushirikiana na Marekani na
kueleza kuwa mchango wake kwa Tanzania ni mkubwa na hivyo inawataka
kujenga ushirikiano zaidi katika sekta za kilimo na nishati.
“Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Hillary Clinton alikuja hapa,
akatupa matumaini ya kuondokana na tatizo la umeme. Tayari wapo
wawekezaji wengi kutoka Marekani ambao wana nia ya kuwekeza katika
nishati,” alisema Dk. Bilal.
Hata hivyo, Makamu wa Rais alisema pamoja na juhudi zote za kuhifadhi
mazingira na viumbe hai, bado Tanzania inakabiliwa na matatizo ya
ujangiri, uvuvi haramu, na magugu maji kufunika kabisa baadhi ya maziwa
na mito.
Naye Seneta Coons alisema katika jimbo lake la Delaware wapo wakulima
wengi ambao wangependa kuja nchini kuwekeza katika kilimo, huku akieleza
Tanzania inavyoweza kuzalisha umeme wa ‘Geothermal’ kwa kushirikiana na
wawekezaji kutoka Marekani.
Chanzo:- http://www.freemedia.co.tz
إرسال تعليق