Tuico wadhalilishwa EPZ

Dar es Salaam. Mgogoro wa malipo kati ya wafanyakazi wa kiwanda cha nguo cha Tanzania Took Garment umechukua sura mpya kutokana na uongozi kutotoa ushirikiano kwa Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na Ushauri (Tuico).
Viongozi hao walifika kiwandani hapo baada ya wafanyakazi wa kiwanda hicho kinachomilikiwa na mwekezaji mwenye asili ya China kugoma kufanya kazi wakidai kuongezewa mshahara.
Katibu msaidizi anayeshughulikia sekta ya viwanda wa Tuico, Thomas Mkolokoti alisema wameshindwa kufikia makubaliano kutokana na dharau waliyo onyeshwa na Wachina hao.
Alisema walifika kiwandani hapo kwa lengo la kuonana na uongozi wa kiwanda ambao haukuonyesha ushirikiano na kuwaambia wafanye wanachokitaka.
“Tulichofanya, tumezungumza na wafanyakazi warejee kazini na madai yao ikiwamo kuomba nyongeza ya mishahara tunayafanyia kazi, ” alisema Mkolokoti.
Baadhi ya wafanyakazi ambao hawakuwa tayari kutaja majina yao walisema kuna mchezo unachezwa na Wachina hao, kwani waliahidiwa kulipwa Sh180, 000, badala ya 100,000 wanayolipwa sasa.
“Waziri wa Viwanda wa China alikuja miezi kadhaa iliyopita na alifanya mkutano hapa hapa kiwandani. Ahadi aliyoitoa ni ya kutaka tulipwe Sh180,000 lakini cha kushangaza hadi sasa tunalipwa Sh100,000 kwa mwezi, ” alisema mmoja wa wafanyakazi hao.
Ofisa rasilimali watu wa kiwanda hicho, Rigobert Masawe alikataa kuzungumzia suala hilo akidai kuwa afuatwe wakati mwingine.
Wakati viongozi wa Tuico wakitaka kuondoka baada ya kumaliza kuzungumza na wafanyakazi, mmiliki wa kiwanda aliwafuata na kuwataka wamwandikie malalamiko hayo kwa maandishi kile walichokubaliana na wafanyakazi, kitu ambacho kilipingwa na viongozi hao.
Huku akitafsiriwa kile kilichokuwa kikizungumzwa na Masawe, Mchina huyo alisema lazima aweke kwenye maandishi huku akimtaka mlinzi aandike kwa madai kuwa anapotakiwa kuwaeleza viongozi wake wa juu, awaeleze kwa maandishi.
“Hatuwezi kukuandikia chochote kwa sababu wakati tunakutaka ukae na sisi kuzungumza, ulikuwa unachezea simu na kutuambia tufanye tunachotaka. Ina maana ulikuwa huna haja ya maelewano. Tumewarudisha wafanyakazi kazini, lakini tunachukua hatua stahiki,” alisema Mkolokoti aliyekuwa akijibizana na Mchina huyo.

Post a Comment

أحدث أقدم