Utafiti: Hali ya uchumi ya mtu mmojammoja nchini ni mbaya kuliko ilivyokuwa miaka 10 iliyopita

Hivi karibuni, Taasisi ya Repoa ilitoa utafiti wake unaoonyesha kuwa hali ya kiuchumi ya wananchi inazidi kuwa mbaya ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka 10 iliyopita.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa, licha ya pato la taifa kuendelea kuongezeka hadi kufikia asilimia saba, Watanzania wengi wanaamini kwamba hali ya uchumi nchini mbaya.
Utafiti huo wa Afrobarometer, awamu ya sita uliofanywa kati ya Agosti 26 na Septemba 29 mwaka jana, walihojiwa Watanzania 2,386 wa Tanzania Bara na Visiwani. Wananchi hao walisema kuwa hali ya maisha inazidi kuwa mbaya ikilinganishwa na ilivyokuwa mwaka 2003.
Akitoa ripoti ya utafiti huo, Dk Lucas Katera kutoka Repoa, anasema wananchi wanalalamika kuwa licha ya Serikali kusema kuwa uchumi ni mzuri na kwamba nchi inapiga hatua ikilinganishwa na ilivyokuwa, wanaona watu wachache tu ndiyo wanaonufaika na maendeleo hayo.
Akitoa mfano anasema mwaka 2003 asilimia 42 walisema hali ya uchumi ilikuwa mbaya, mwaka 2005 asilimia 38, utafiti uliofuata mwaka 2008 idadi ya wananchi iliongezeka na kufikia asilimia 57 huku mwaka jana walikuwa asilimia 67.
“Idadi ya wananchi wasioridhishwa na namna Serikali inavyotekeleza miradi ya huduma za kijamii imeongezeka. Wananchi wanne kati ya kumi hawafurahishwi na huduma ya maji inayotolewa,” anasema Dk Katera.
Mtafiti huyo anasema matokeo hayo yamebaini kuwa kuna uhusiano wa karibu kati ya hali mbaya ya kiuchumi na utoaji mbaya wa huduma za jamii.
“Wananchi saba kati ya kumi wanasema Serikali inafanya vibaya kwenye sekta ya maji na elimu jambo linalosababisha hali mbaya ya kichumi,” anasema.
Mtaalamu wa Sera na Bajeti, Gilead Teri anasema wananchi wanahoji juu ya sababu zinazofanya matumizi ya Serikali kutowekwa wazi. Wanapendekeza uwazi zaidi uongezwe kwenye masuala yanayohusu umma.
“Wengi wamekata tamaa, wanasema takwimu hizo haziendani na hali halisi ya kipato chao. Hapa Serikali inapaswa kuchukua hatua ikiwa ni pamoja na kuboresha huduma za jamii,” anasema.
Teri anasema kukithiri kwa rushwa ni moja ya changamoto zinazowafanya wananchi kutokuwa na imani na Serikali.
Mtaalamu wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Prosper Ngowi anasema uchumi unaweza kukua, lakini kama hakutakuwa na matumizi sahihi ya fedha za umma wananchi wataendelea kuona kasoro za kiuchumi.

Post a Comment

أحدث أقدم