Ada Elekezi Shule Binafsi Tayari



TUME ya wataalamu waliokuwa wanakusanya maoni ya wadau wa elimu na kukokotoa ada elekezi kwa shule za msingi na sekondari zisizo za Serikali, wamemaliza kazi yao na tayari wamekabidhi ripoti hiyo kwa Serikali.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Sifuni Mchome amethibitisha kukamilika kwa kazi hiyo na sasa kinachofuata ni uchambuzi wa ripoti pamoja na kuangalia miongozo ya Serikali kabla ya ada elekezi kutangazwa na kuanza kutumika kwa majaribio mwakani Januari.
Wataalamu hao walipewa kazi na Serikali kuandaa ada elekezi baada ya kupata maoni ya wadau mbalimbali wa elimu wakiwemo wazazi, wananchi, wamiliki wa shule binafsi, walimu, asasi zisizokuwa za kiserikali, taasisi mbalimbali za umma na wadau wengine ambao wanaweza kusaidia katika ukokotoaji huo wa ada.
Katika ukokotoaji huo, wizara inaandaa mchanganuo wa gharama za kumsomesha mwanafunzi kuanzia elimu ya awali, darasa la kwanza hadi kidato cha sita kwa nia ya kutoa ada hiyo elekezi ambazo zitaendana na huduma itolewayo kwa shule zisizo za Serikali.
Alisema shule zitakazoteuliwa kuanza kutumika kwa ada hizo zitatangazwa pia na wizara hiyo baada ya kukutana na wamiliki wa shule hizo na kufanya nao mazungumzo.
Alisema majaribio hayo yatafanyika katika baadhi ya shule Tanzania nzima na sio katika baadhi ya mikoa tu.

Post a Comment

Previous Post Next Post